Hee! Kumbe BUKAYO Saka anaitamani Liverpool

Hee! Kumbe BUKAYO Saka anaitamani Liverpool

LONDON ENGLAND.  HAYA sasa, nyota anayekipiga Arsenal, Bukayo Saka pamoja na wawakilishi wake wamevutiwa na klabu ya Liverpool na huenda Mwingereza huyo akajiunga nayo siku za usoni, kwa mujibu ripoti za chinichini.

Saka, 20, ni kati ya mchezaji muhimu ndani ya klabu ya Arsenal na ametabiriwa ataendelea kukipiga humo kwa muda mrefu.

Hata hivyo, mbali na Saka na wawakilishi kuonyesha kuvutiwa na Liverpool kwa mujibu wa ripoti, kocha anayeinoa timu hiyo ya Anfield, Jurgen Klopp naye amemfuatilia kinda huyo kwa muda mrefu.

Sasa kwa mujibu wa maelezo ya chini ya kapeti yaliyoripotiwa na McGarry, Saka huenda akafungua njia ya kujiunga na Liverpool siku za usoni.

Hata Hivyo, McGarry alisema Arsenal kwa sasa inahaha kuhakikisha inamwongeza mkataba mpya na tayari wameshaanza mazungumzo na wakala wa Saka, kuhusu mkataba huo ambao utamalizika mwaka 2024.

“Nadhani Liverpool watamtengenezea Saka mazingira ya kujiunga nao na kucheza soka la kiwango cha hali ya juu, hili ni jambo ambalo nimepewa taarifa na wawakilishi wamevutiwa na mipango hiyo,” alisema McGarry.

Saka ameonyesha kiwango bora msimu huu na ameshacheka na nyavu mara tano kwenye Ligi Kuu England na kuwa mchezaji muhimu ndani ya kikosi cha Mikel Arteta msimu huu.

Kinda huyo alikuwa pia kinara kwenye mechi ya Ligi Kuu England dhidi Norwich City wikiendi iliyopita kwani alitoa asisti yake ya nne katika ushindi wa mabao 5-0 waliopata.