Mastaa Gor kuhepea Police

Mastaa Gor kuhepea Police

HUKU dirisha la usajili likiwa wazi, mibabe wa soka Gor Mahia wameanza kupaniki wakihofia kuwapoteza wachezaji wao nyota.

Kwa zaidi ya miaka mitano sasa, Gor imekuwa ikiwapoteza mastaa wake kutokana na kushindwa kuwazuia wasiondoke kwa sababu ya hali yao ya msoto.

Ndio hali wanayopitia sasa hivi baada ya mastaa wawili wa kikosi cha kwanza kudaiwa kuwa wapo mbioni kujiunga na Police FC.

Police FC wameingia kwenye ligi msimu huu kwa vishasha wakimwaga pesa za kutosha kusajili wachezaji nyota.

Sasa wanaripotiwa kuwa mbioni kumnasa beki wa kati Philemon Otieno na kiungo beki Ernest Wendo ambaye kajaza pengo la Kenneth Muguna aliyewatoka Gor kwa dizaini hiyo na kujiunga na Azam ya Tanzania.

Wawili hawa wamesusia mechi kadhaa za mwisho za Gor, Wendo akiwa tayari amevunja mkataba wake nao baada ya kukosa kulipwa mshahara wake wa zaidi ya miezi mitatu.

Naye Otieno kagoma kusaini mkataba mwingine baada ya ule aliokuwa nao kufika tamati Disemba 2021.

“Kocha (Bobby Ogolla) kweli ameelezea matamanio yake ya kuwanasa wawili hao. Yupo makini sana kukirutibisha ngome ya ulinzi akiwa ameipa kipau mbele,” mdokezi kutoka Police FC kafichua.

Ogolla aliwahi kuwa naibu kocha Gor. Amewahi kumfunza Wendo ambaye pia anaweza kutumika kama beki wa kati pale panapokuwa na ulazima.

Otieno naye kando na kucheka kama sentahafu, ana uweledi pia wa kucheza kama fulubeki. Sifa hizi ndizo zinamfanya Ogolla kupambana kuwanasa.

Mwanzoni mwa msimu huu Ogolla alifanya usajili mzito wa mastaa wakali akiwemo Duncan Otieno beki Musa Mohammed, straika John Makwatta, Duke Abuya na wing’a Clifton Miheso. Miheso alitokea Gor baada ya kudinda kusaini mkataba mpya nao.