Yanga yauona mwezi baada ya dakika 270

Yanga yauona mwezi baada ya dakika 270

Muktasari:

  • Baada ya kukosa mabao ndani ya dakika 270 Yanga leo imeona mwezi kwa kuifunga Dodoma Jiji mabao 2-0 kwenye uwanja wa Jamhuri.

BAO la kideo la Dikson Ambundo na Mohamed Yusuf kipa wa Dodoma ambaye alijifuinga yalitosha kuendelea kuipa uongozi Yanga kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC wakifikisha pointi 60 na kuwaacha Simba nyuma kwa pointi 11.

Baada ya kukosa mabao ndani ya dakika 270 Yanga leo imeona mwezi kwa kuifunga Dodoma Jiji mabao 2-0 kwenye uwanja wa Jamhuri.

Yanga ilianza mchezo kwa kuliandama zaidi lango la Dodoma jiji na kutumia dakika 11 kupata bao la utangulizi likifungwa na Dikson Ambundo ambaye alipiga shuti nje ya 18 akipokea pasi kutoka kwa Jesus Moloko na kumuacha kipa Yusuf akiruka bila mafanikio.

Yanga walitawala mpira eneo la kiungo ambalo lilisimamiwa vyema na Salum Abubakari 'Sure Boy' huku wakitumia mawinga zaidi kupeleka mipira kwa wapinzani wao kutokana na kasi yao.

Kipindi cha kwanza Yanga walichonga kona tatu zote hazikuwa na madhara langoni kwa wapinzani wake huku ndani ya dakika hizo Dodoma Jiji hawakupata kona hata moja.

Dakika ya 23 kipa wa Yanga, Djigui Diarra alipata kashikashi baada ya Feisal Salum 'Fei Toto' kumfanyia madhambi Emmanuel Martin na mwamuzi Ramadhan Kayoko kuamuru faulo kupigwa kuelekwezwa lango la Yanga mpira ambao ulikuwa unaenda kuleta madhara lakini kutokana na umakini wa kipa aliuokoa.

Yanga walijibu shambulizi dakika ya 35 kupitia kwa kiungo Zawadi Mauya ambaye alipiga shuti nje ya 18 ambalo lilionwa na kipa Yusuf ambaye alishindwa kuudaka na kuukwamisha nyavuni mwenyewe.

Hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika Yanga waliondoka kifua mbele uwanjani kwa mabao 2-0 huku kadi moja tu ya njano ikitolewa kwa Djuma Shaban dakika ya 29.

Kipindi cha pili Dodoma Jiji walikubali kufunguka lakini hawakuwa na madhara kutokana na uimara wa kipa wa Yanga ambaye aliokoa mashuti matatu langoni mwake kama si ubora wake basi yangekuwa yanazungumzwa mengine.

Dodoma Jiji kipindi cha pili waliruhusu mpira kuchezwa tofauti na dakika 45 za kipindi cha kwanza ambacho walikuwa wanatumia mipira mirefu kidogo ilisaidia na kumpa kashikashi Diarra ambaye alikuwa hana kazi langoni kwake.

Dakika ya 59 Dodoma walifanya mabadiliko kwa kumtoa George Wawa na nafasi yake ilichukuliwa na Erick Nkosi alitoka Nassoro Maulid aliingia Salmin Hoza.

Mabadiliko yao yaliongeza uhai japo ubora wa mchezaji mmoja mmoja kuhakikisha hawaruhusu nyavu zao zinatikiswa, huku Yanga wao wakiendelea kusaka mabao lakini mabeki wa timu pinzani waliongeza uimara wa kulinda.

Dakika ya 67 Yanga walipata kona ikichongwa na Ambundo shuti lake lilikuwa mboga kwa kipa wa Dodoma, dakika ya 69 Dodoma walijibu kwa kupata kona Maulid na kupanguliwa na kipa na kuzaa kona nyingine ambayo ilidakwa na kipa Diarra.

Dakika ya 77 yanga walifanya mabadiliko kwa kumtoa Fei Toto na nafasi yake kuchukuliwa na Yanick Bangala na alitoka Moloko nafasi yake ilichukuliwa na Denis Nkane.

Dakika ya 80 Nkane akiwa ndani ya 18 ameshindwa kuiandikia timu yake bao la tatu baada ya shuti lake kugonga mwamba na kurudi ndani ya uwanja.
dakika ya 88 Mayele alitoka nafasi yake ilichukuliwa na Makambo wakati Machezo alitolewa nje kwa kadi nyekundu baada ya kucheza rafu Yanick Bangala.

Kikosi cha Yanga; Djigui Diarra, Kibwana Shomari, Dickson Job, Bakari Mwamnyeto, Djuma Shabani, Zawadi Mauya, Salum Abubakar 'Sure Boy', Jesus Moloko, Dickson Ambundo, Feisal Salum 'Fei Toto' na Fiston Mayele

Dodoma Jiji; George Wawa, Paul Ngalema,Joram Mgeveke, Agustino Msata, Salmin Hoza, Rajabu Seif Mgalula, Cleophas Mkandala, Anuary Jabir, Wazir Junior na Emanuel Martin.