Yanga waondoka uwanjani

DAKIKA 15 pekee ziliwatosha Yanga kusubiri kuanza kwa mchezo wao dhidi ya Simba na baada ya kuona hakuna timu wala waamuzi wanaoingia uwanjani hapo waliondoka na kurudi katika vyumba vya kubadilishia nguo.

Wakati wanaondoka majukwaa yaliyokuwa ma mashabiki wa timu hiyo yaliinuka kwa shangwe na kuishangilia timu yao huku wengine wakiondoka uwanjani hapo.

Ilipofika saa 11:35 wachezaji wa Yanga walitoka vyumbani na kupanda gari lao na kisha waliondoka uwanjani.

Wakati gari likitoka uwanjani mashabiki walikuwa wakiswasindikiza huku wakiimba “TFF, TFF ”, na kulifata gari kwa nyuma.

Baada ya Yanga kuondoka uwanjani hapo, mashabiki wa Simba walionekana kupoa huku wale wa Yanga wakiendelea kushangilia na kuondoka uwanjani hapo mdogo mdogo.

Huenda yote hayo yamesababishwa  na Shirikisho la soka Tanzania ‘TFF’ ambao wamebadili muda wa mechi masaa matatu kabla ya mchezo huo  kuanza.

Hapo awali mechi hiyo ilipangwa kupigwa Leo saa 11:00 lakini mchana wa saa  nane ilitoka ratiba ya kusogeza mechi hiyo mbele hadi saa 1:00 usiku.

Yanga walionekana kutokubaliana na uamuzi huo kwani walifika mapema saa kumi na kupasha kisha kurejea vyumbani kubadili jezi na kuingia kwaajili ya mtanange kuanza saa 11:00.


SIMBA WAWASILI

Gari la Simba ambalo lilibeba wachezaji lilifika uwanjani hapo saa 11:20, hivyo mashabiki wa Yanga walisogea karibu na eneo hilo wakiimba TFF.
Hivyo ilikuwa ni kama mashindano nao mashabiki wa Simba walisogea kujibizana nao.
Wakati matukio hayo yakiendelea askari wa kulinda usalama wao walikuwa imara kusimamia usalama ili wasiumizane.