Yanga haipoi Makambo, Nkane watakata

Yanga haipoi Makambo, Nkane watakata

Unguja. YANGA ikiwatumia nyota wao wapya waliowasajili Denis Nkane pamoja na staa wa Haritier Makambo wameonyesha ubora wao kuwa hawabahatishi na kuifungia timu yao mabao 2-0.

Yanga wamecheza na Taifa Jang'ombe ikiwa ni mechi yao ya kwanza ya Kombe la Mapinduzi mashindano yanayoendelea Uwanja wa Amaan kisiwani hapa.

Makambo ndiye alianza kutikisa nyavu za wapinzani wao dakika ya 32 akipiga shuti la mbali lililomshinda kipa wa Taifa Jang'ombe Hussein Abel.

Wakati Makambo akifunga bao hilo Denis Nkane alitikisa nyavu za wapinzani wao dakika ya 49 huku akikosa bao lingine dakika ya 56 ambapo shuti lake lilitoka nje ya goli.

Nkane aliyesajiliwa akitokea Biashara United ameonekana kuwa bora wakati wote wa mchezo huo huku akisumbua ngome ya wapinzani wao.

Taifa Jang'ombe walionekana kushambuliwa zaidi kipindi cha kwanza ingawa dakika ya 27 Yanga ililishambulia lango la wapinzani wao ingawa nao walifanikiwa kunusuru hatari hiyo langoni mwao na kumpa kazi nzito kipa wa Taifa Jang'ombe kuokoa mashambulizi yao.

Hata hivyo, Taifa Jang'ombe walijitahidi kupambana na wapinzani ambao hii ndio mechi yao ya kwanza ya Kombe la Mapinduzi huku kiungo mpya Abubakar Salum 'Sure Boy' akilishika vyema dimba la kati.

Kwa upande wa kipa wa Yanga, Aboutwalib Mshery hakupata kashikashi nyingi kutoka kwa wapinzani wake kwani ngome yake ya ulinzi chini ya Nahodha Bakari Mwamnyeto ilionekana kuwa imara zaidi huku Deus Kaseke akiikosesha timu yake bao dakika ya 79 baada ya kupiga shuti lililogonga mwamba na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda.

Taifa Jang'ombe hii ni mechi yao ya pili baada ya ile ya awali kufungwa na KMKM bao 2-1 ambapo Yanga itacheza mechi yao pili Ijumaa na KMKM.

Makocha wa timu hizo Cedric Kaze wa Yanga na Omar Khamis wa Taifa walifanya mabadiliko ya vikosi vyao ambapo Yanga alitolewa nje Dickson Ambundo/Crispin Ngushi ambaye amesajiliwa hivi karibuni akitokea Mbeya Kwanza pamoja na Nkane/Mapinduzi Balama

Upande wa Taifa waliotoka ni Ahmed Mohamed/Khelef Saleh, Ali Makelele/Azak-rabin Mbarouk, Jamal Abdul/Joshua Salum, Yasir Masoud/Peter Stanley, Adil Nasor/Abdalla Mudhihir.