Ujio wa Chama wamkuna Pablo

KOCHA Mkuu wa Simba, Pablo Franco.

UJIO wa kiungo fundi wa klabu ya Simba, Clatous Chama umemkosha Kocha Mkuu wa klabu hiyo Pablo Franco na kukiri ataisaidia timu yake.

Chama amerejeshwa Simba kwa kandarasi ya miaka miwili baada ya kushindwa kuendelea katika maisha yake nchini Morocco.

Katika mazungumzo na Mwanaspoti, Pablo alisema ujio wa Chama una tija kubwa kwa timu yake kutokana na uwezo wake.

Alisema alipomuona Chama katika video mbalimbali alikubati uwezo wake na ndio maana hakutaka kuweka kikwazo katika urejeo wake.

“Ni mchezaji mzuri sana, naamini ataisaidia timu kwa kushirikiana na wenzake, uwezo anao mkubwa tu na nina imani naye,” alisema Pablo.

Pablo alisema hata katika mitandao mbalimbali ya kijamii amekuwa akifuatilia na kuona namna ambavyo mchezaji huyo amekuwa akizungumza na hiyo yote inachagizwa na uwezo wake mkubwa alionao.

“Angekuwa mchezaji wa kawaida asingezungumzwa kiasi kile ilinifanya hata mimi kumfuatilia sana ili kuona uwezo wake, “alisema Pablo.

Pablo alisema kila mchezaji ambaye yupo Simba anauwezo na ndio maana kasajiliwa hivyo anaamini malengo yatatimia kwa timu aliyonayo.


UBINGWA MAPINDUZI

Pablo alisema amekoshwa na namna wachezaji wake walivyopambana kulitwaa taji hilo ambalo kwake ni la kwanza toka ajiunge Simba.

“Nimefurahi sana kupata ubingwa wa Mapinduzi kwangu ni jambo kubwa Sana lakini pongezi zaidi kwa wachezaji wangu,” alisema Pablo aliyewataka wanachama wa Simba kuendelea kuisapoti timu yao katika kila mashindano ambayo itayashiriki ili kufikia malengo ya kila kombe wanalowania.


BOCCO ATEMA NYONGO

Nahodha wa Simba, John Bocco amesema haikuwa rahisi wao kutwaa taji la Mapinduzi dhidi ya Azam FC ubora na uzoefu wa wachezaji wao ndio siri ya mafanikio.

Simba wametwaa taji hilo baada ya kumfunga Azam FC bao 1-0 iliwa ni fainali yao ya tatu kukutana na wao kuibuka na ubingwa baada ya kushindwa mara mbili.

Bocco alisema kwenye mchezo huo wapinzani wao walikuwa bora kipindi cha kwanza na wao kipindi cha pili alitumia nafasi hiyo kuwapongeza wachezaji wenzake kwa kupambana na kuwaambia kuwa ni mwanzo wanahitaji mataji zaidi.

“Azam FC walicheza vizuri lakini hawakuwa bora kama tulivyokuwa bora kitu kilichosaidia sisi kupata matokeo ambayo yametupa taji la nne,” anasema Bocco na kuongeza;

“Habari za taji sasa tumelisahau tunaangalia namna ya kutetea taji la ligi kuu ambalo tumelitwaa mara nne mfululizo na tunaimani tunaweza kutokana na matarajio na morali kwa wachezaji.”