Simba yabanwa mbavu na Geita Gold, Mpole atetema

Simba yabanwa mbavu na Geita Gold, Mpole atetema

Mwanza. MCHEZO wa Ligi Kuu bara kati ya Geita Gold FC dhidi ya Simba SC umemalizikwa kwa timu hizo kutoka sare 1-1 kwenye uwanja wa CCM Kirumba.

Kwenye mchezo huo Geita Gold ilikuwa ya kwanza kupata bao lililofungwa na straika wake, George Mpole likadumu kwa dakika nane kisha Kibu Denis akaisawazishia Simba dakika ya 27.

Pamoja na juhudi za washambuliaji wa timu zote kuonyesha njaa ya kufunga mabao hadi dakika 45 zinamalizika matokeo yalikuwa sare 1-1.

Kipindi cha pili kilianza kwa Simba kuanza mpira kwa kasi huku Geita Gold wakionekana kuyamudu mashambulizi ya wapinzani wao.

Ilipofika dakika ya 60 kocha wa Simba Pabro Franco alifanya mabadiliko kwa kumtoa John Bocco nafasi yake ikichukuliwa na Meddie Kagere, Gadiel Michael akaingia Mohamed Hussein na Thadeo Lwanga ambaye nafasi yake imechukuliwa na Erasto Nyoni.

Mabadiliko hayo yalionekana kuleta uhai kwa kikosi cha Simba japo Geita Gold iliyamudu ndipo Pablo alipofanya mabadiliko mengine dakika ya 75 kwa kumtoa Sadio Kanoute na nafasi yake kuchukuliwa na Peter Banda.

Kwa upande wake Kocha wa Geita, Fred Minziro dakika ya 70 alimtoa, offen Chikola ambaye nafasi yake imechukuliwa na Amos Kadikilo.

Mashambulizi yalidumu muda wote katika pande zote huku Geita Gold wakionekana kulinda lango lao kwa nidhamu na kuifanya mchezo huo kumalizika kwa sare 1-1.