Simba ubingwa wa 4 mabao 4

Simba imekamilisha msimu wa 2020/21 kwa utamu wakiipiga Namungo ya Lindi kwa mabao 4-0 katika mchezo wa mwisho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Walichofanya Simba ni kunogesha ubingwa wao wa nne mfululizo wakishinda kwa kishindo bao 4-0 katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.
Mchezo ulianza kwa Simba kufanyiwa mapokezi ya kibingwa ambapo Namungo walijipanga katika mistari miwili huku wekundu hao wakipita katikati huku wakipigiwa makofi na wageni wao pamoja na mashabiki.

Simba ndio waliouanza mchezo kwa kasi na dakika ya 5 tu wanatengeneza shambulizi zuri lakini shuti la mshambuliaji Chris Mugalu linazuiwa na beki Steven Duah mpigaji akipokea pasi safi ya kiungo Clatous Chama.

Simba walifanya shambulizi lingine zuri dakika ya 12 pasi ndefu ya winga Luis Miquissone inamkuta beki wake wa kishoto Mohammed Hussein 'Tshabalala' akiwa ndani ya eneo la hatari lakini shuti lake linadakwa vyema na kipa Jonathan Nahimana.
Namungo wanajipanga na kufanya mashambulizi mazuri dakika ya 16 la kwanza pasi ya mshambuliaji Reliant Lusajo inamkuta kiungo Lucas Kikoti akiwa ndani ya eneo la hatari lakini shuti lake linapanguliwa vizuri na kipa Aishi Manula.
Wakati Simba wakiokoa Namungo wanaunasa tena mpira lakini krosi ya beki wao wa kulia Haruna Shamte inakosa mmaliziaji.

Simba walifanikiwa kupata bao la kuongoza dakika ya 18 likifungwa na mshambuliaji Meddie Kagere akimzunguka beki wa Namungo kisha kufunga kwa mguu wa kushoto akipokea pasi safi ya mwenzake Mugalu ambaye alitangulia kufanya kazi nzuri ya kumzidi nguvu na kasi beki wa Namungo Japhary Mohammed.

Wakati Namungo wakijiuliza wakajikuta wanafungwa bao la pili dakika ya 25 mfungaji akiwa Mugalu akimalizia pasi safi ya beki wake wa kulia Shomari Kapombe.

Dakika ya 34 Nahimana anafanya kazi nzuriakipangua shuti la Chama shambulizi la mpira wa adhabu ndogo na kuwa kona ambayo hata hivyo haikuwa na madhara.
Simba wanatawala mchezo wakipiga pasi wanavyotaka na kutawala huko mchezo dakika ya 39 almanusura wapate bao la tatu shuti la Kagere linapanguliwa na miguu ya Nahimana na kuwa kona mpigaji akipokea pasi safi ya Chama.
Dakika ya 40 Namungo wanaamua kubadilisha silaha wakifanya mabadiliko mawili kwa pamoja wakimtoa Hashim Manyanya nafasi yake ikichukuliwa na Abeid Athuman huku pia wakimtoa Erick Kwizera nafasi yake ikichukuliwa na Shiza Kichuya.

Miquissone anapoteza nafasi nzuri kuipa timu yake bao la nne shuti lake la mguu wa kulia linatoka nje kidogo akipokea pasi ya Chama.

Dakika ya 45 Namungo wanapiga shuti la pili lililolenga lango likipigwa na Shamte lakini linadakwa vyema na Manula.
Mpaka mapumziko Simba ilitoka inaongoza kwa mabao 2-0 huku pia wakionekana kutawala mchezoKipindi cha pili Simba walirejea na kasi ya kusaka mabao zaidi na dakika ya 50 tu Mugalu anapoteza nafasi nzuri mpira unatoka nje kidogo akipokea pasi ya Kagere.
Dakika ya 57 Namungo wanatengeneza shambulizi zuri lakini shuti la Kagere Athuman linatoka nje kidogo.
Dakika ya 68 Simba walifanikiwa kupata la tatu likifungwa na Mugalu ambaye alifunga bao lake la pili katika mchezo akimalizia kirahisi pasi ya yuleyule Kapombe aliyemtengenezea bao la kwanza.
Bao hilo liliwafanya Namungo kumzonga mwamuzi  Nassoro Mwinchui kutoka Tanga wakidai kabla ya bao hilo Miquissone hakuwa sahihi katika kuanza haraka mpira wa adhabu.
Dakika ya 69 Namungo walifanya mabadiliko wakimtoa Hamis Khalifa nafasi yake ikichukuliwa na Stephen Sey lakini pia Simba nao dakika ya 70 wakimtoa Rally Bwalya ambaye alikuwa ndio mwiba wa Namungo katika eneo la kati nafasi yake ikichukuliwa na nahodha wao mkuu John Bocco.
Simba walifanya mabadiliko mengine katika safu ya ulinzi wakimtoa beki Mohammed Ame dakika ya nafasi yake ikichukuliwa na Kennedy Juma.
Simba walionekana kutawala mchezo pia kipindi cha pili wakicheza pasi zinazofika
Dakika ya 82 Simba wanafanya mabadiliko mengine wakimtoa Chama nafasi yake ikichukuliwa na Hassan Dilunga.
Simba ilifanikiwa kupata bao la nne kwa njia ya penalti ikifungwa na Bocco akimchambua vizuri Nahimana.
Penalti hiyo ilitokana na Bocco mwenyewe kuangushwa ndani ya eneo la hatari na Duah wakati akitafuta nafasi ya kwenda kufunga.
Mpaka mwisho wa mchezo Simba ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 4-0 na kunogesha sherehe zao za ubingwa wa nne mfululizo.