Simba imevuna ilichopanda

Muktasari:

MABOSI wa Simba wamewatuliza mashabiki wao na kuwaambia sare waliyopata kwa Biashara United ni mavuno ya kile walichopanda na wasahau sasa ili waelekeze nguvu kwenye mechi zao zijazo ikiwamo ya leo dhidi ya Dodoma Jiji.

MABOSI wa Simba wamewatuliza mashabiki wao na kuwaambia sare waliyopata kwa Biashara United ni mavuno ya kile walichopanda na wasahau sasa ili waelekeze nguvu kwenye mechi zao zijazo ikiwamo ya leo dhidi ya Dodoma Jiji.

Mwenekiti Mpya wa Bodi ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba, Abdallah Salim ‘Tray Again’ ndiye aliyesema hayo ikiwa ni siku chache tangu akivae cheo hicho baada ya Mohammed ‘Mo’ Dewji kujiuzulu juzi.

Akizungumza na Mwanaspoti, Try Again alisema wanasimba hawapaswi kuumia au kusononeka kwa suluhu katika mechi yao ya kwanza kwani wamevuna walichopanda na waelekeze nguvu kwa mechi zijazo.

“Simba itaendelea kuwa juu na bora wakati wote, tumetoka pre-season (maandalizi ya msimu mpya) halafu tukaja kucheza na Mazembe, Yanga na Biashara hizo zote ni kama kuangalia kiwango, hivyo hakuna sababu ya watu kupaniki, ndivyo soka lilivyo tujipange kwa mechi nyingine,” alisema Try Again na kuongeza;

“Sasa tuiangalie Simba baada ya mechi tano hadi sita za ligi itakuwaje hapo ndipo waanze kuijadili, ila kwa sasa sisi kama viongozi tumeridhika na tulichokipata katika mchezo wa kwanza.”

Aidha Try Again alisisitiza wanaimani kubwa na benchi zima la ufundi chini ya Didier Gomes na wasaidizi wake sambamba na wachezaji wote wakiwamo waliokuwapo na wale wapya na kutaka wanasimba washikamane ili kuendelea kupata raha kama za misimu minne mfululizo iliyopita.