Rais Samia aongoza waombolezaji kuuaga mwili wa Teddy Mapunda

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameongoza maelfu ya waombolezaji kuaga mwili wa mfanyabiashara na mkurugenzi wa kampuni ya Montage, Teddy Mapunda aliyefariki dunia Mei 6, 2021.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameongoza maelfu ya waombolezaji kuaga mwili wa mfanyabiashara na mkurugenzi wa kampuni ya Montage, Teddy Mapunda aliyefariki dunia Mei 6, 2021.

Ibada ya kuaga mwili huo inafanyika leo Jumapili Mei 9, 2021 katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.

Viongozi wengine walioshiriki ibada hiyo ni Rais mstaafu wa awamu ya nne Jakaya Kikwete, Mkuu wa Jeshi la Polisi Simon Sirro, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar Kate Kamba.

Akizungumza wakati wa ibada hiyo mume wa marehemu Nestory Mapunda alimuelezea mkewe kama mwanamke mpambanaji aliyejitoa kwa dhati kufanya shughuli mbalimbali za serikali na CCM.

“Wakati wa kampeni yeye alizunguka na mgombea urais, mie nilikuwa na mgombea mwenza tulifanya kazi katika mazingira yote, kwangu hadi sasa imekuwa vigumu kuamini kuwa ametuacha ila sina cha kufanya zaidi ya kushukuru. Teddy your one piece in town, nakupenda,” amesema Mapunda.