Mugalu, Mhilu kuwakosa Watswana

Mshambuliaji wa Simba, Chris Mugalu ataukosa mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Jwaneng Galaxy ya Botswana kutokana na kukabiliwa na majeruhi ya nyama za paja.
Simba inatarajia kuondoka kesho mchana kwenda Botswana tayari kwa mchezo huo.
Kocha Didier Gomes amesema Mugalu hatakuwa sehemu ya mchezo huo kwani hajafanya mazoezi na wenzake.
"Ana majeruhi na hayupo mazoezi hivyo hataweza kusafiri na timu. Aliumia mazoezini wakati tukijiandaa na mechi na Biashara na hakucheza mchezo huo lakini tukamchezesha mechi iliyofuata ya Dodoma Jiji na akajitonesha," alisema Gomes.
" Pia katika mchezo huo tutamkosa Yusuf Mhilu ambaye alichelewa kwenye usajili wa kimataifa," amesema Gomes.
Gomes amesema hana shaka juu ya kikosi chake kwani kimejiandaa vizuri kushinda mchezo huo ili kutimiza malengo yao ya kutinga hatua ya makundi ya mashindano hayo na kufika mbali zaidi.
"Tumejiandaa vizuri hasa kuhakikisha tunacheza kwa haraka kupata mabao ya mapema,lakini tukiongeza umakini katika kujilinda, Ili tusiruhusu bao" amesema Gomes.
Amesema wachezaji wengine wawili katika kikosi chake, Duncan Nyoni na Peter Banda wanatarajia kuwasili leo usiku na kesho asubuhi wataungana na wenzao mazoezini kabla ya kusafiri kwenda Botswana.