Morisson azomewa kwa Mkapa

MSHAMBULIAJI wa Simba, Bernard Morisson amejikuta katika wakati mgumu baada ya kuzomewa na mashabiki wa Yanga katika mchezo wao dhidi ya Yanga ukiendelea kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa.

Kuzomewa kwa Morrison ni baada ya kocha wa Simba, Pablo Franco kumtoa dakika 54 na nafasi yake akiingia Kibu Denis wakati huo huo Sadio Kanoute alishindwa kuendelea na mchezo baada ya kuumia na nafasi yake kuchukuliwa na Mzamiru Yassin.

Muamuzi msaidizi wa nne Elly Sasii aliponyanyua kibao cha kubadilisha wachezaji ilipoonekana namba ya Morrison mashabiki wa Yanga walianza kumzomea.

Mchezaji huyo hakuonyesha kujali kwani alitoka bila kuwa na presha yoyote huku akiwa ameinamisha kichwa chini.

Morrison katika mchezo huo alikuwa na wakati mgumu chini ya Kibwana Shomari na hata alipohama upande kwenda kulia alikutana na mabeki Djuma Shaban na Dickson Job.