Makocha Bongo wamteta Solskjær

SIKU mbili baada ya Manchester United kuachana na Ole Gunnar Solskjaer, makocha nchini wamemzungumzia kocha huyo raia wa Norway.

Man U iliachana na kocha huyo saa chache baada ya kipigo cha mabao 4-1, kwenye mechi ya Ligi Kuu England.

Uamuzi huo umepokelewa kwa mitizamo tofauti na baadhi ya makocha nchini, wengine wakisema timu hiyo ilikuwa kubwa kuliko uwezo wa kocha na wengine wakiamini alishindwa kuendana na falsafa za klabu.

Kocha Francis Baraza wa Kagera Sugar anasema; “Walimpa muda kuona kama atabadilisha mwenendo wa timu, ila presha kubwa ilitoka kwa mashabiki na ndiyo wamepelekea kufukuzwa.”

Alisema mechi na Liverpool ilikuwa na presha kwa kuwa ni dabi. “Ni bora Manchester ifungwe na timu nyingine lakini si Liver au Man City, hivyo moja ya mechi zilizomuondoa ni hiyo.”

“Naikumbuka mechi yao na Bayern Munich Ole Gunner aliweka historia na klabu ilitarajia ataweza kurudisha zama za Sir Alex lakini imekuwa tofauti”

Kocha Seleman Matola alisema Ole Gunnar; “Kwake ilikuwa ngumu japo alijaribu, ameshindwa kuendana na falsafa ya klabu,” alisema Matola kauli sawa na iliyotolewa na Zuberi Katwila wa Ihefu.

“Manchester walimuamini kwa kuwa ni mzawa pale na kizazi cha Sir Alex, hivyo walitarajia angeendeleza falsafa ya klabu

“Ule uzawa na kucheza pale klabu ilifahamu ni mtu sahihi, ingawa ilikuwa ni kama kucheza bahati nasibu na falsafa yao imefeli kwa mtu wao wa ndani,”alisema.

Solskjaer alikingiwa kifua mara kwa mara na Sir Alex Ferguson, ingawa sasa klabu itamlipa Pauni 7.5 milioni kama fidia.

Ikumbukwe Solskjaer alisaini mkataba wa miaka mitatu. Man United imefungwa mechi saba katika mechi 13 walizocheza msimu huu.

Sasa kiungo zamani wa timu hiyo Darren Fletcher, atakuwa kocha wa muda hadi mbadala wa Solskjaer atakapotikana.

Fletcher ataiongoza Man United akisaidiana na Michael Carrick kuelekea mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi Villarreal kabla ya kumenyana na Chelsea wikiendi ijayo.

Zinadine Zidane anapewa nafasi kubwa ya kuchukua mikoba ya Solskjaer endapo kama atakubali.