Mabosi Simba wavamia mazoezi

Mabosi Simba wavamia mazoezi

ZIKIWA zimebaki siku mbili Simba irushe karata yake ya kwanza kwenye Kombe la Shirikisho Afrika msimu huu dhidi ya Red Arrows ya Zambia, mabosi wa timu hiyo wametinga mazoezini kuangalia kinachoendelea.

Katika mazoezi ya leo jioni yanayoendelea kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Mwanaspoti limemshuhudia Mtendaji Mkuu wa timu hiyo Barbara Gonzalez akiwasili uwanjani hapo huku akiambatana na vigogo wengine wa timu hiyo.

Viongozi wa Simba wakiongozwa na Salim Abdallah 'Try Again' wakijadiliana jambo pamoja na Waziri wa Nishati, January Makamba jioni ya leo katika mazoezi ya Simba yanayofanyika uwanja wa Benjamin Mkapa. Picha|Loveness Bernad

Barbara aliingia uwanjani hapo akiambatana na baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’, Murtaza Mangungu, Mwina kaduguda, Hussein Kitta na Mulam Nghambi.

Viongozi hao walipofika walikaa kwenye mabechi yaliyopo uwanjani hapo katika eneo la kukimbilia na kuendelea kuangalia mazoezi huku wakipiga stori tofauti tofauti.

Simba ndio timu pekee ya soka iliyobaki ikiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya Kimataifa baada ya Azam, Biashara United na Yanga kutolewa na mchezo dhidi ya Arrows utapigwa Jumapili saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa Mkapa.