KMC kutesti silaha kwa wajeda

KIKOSI cha KMC kinachonolewa na kocha Habib Kondo leo kitacheza mchezo wa kirafiki na klabu ya JKU ya Zanzibar mchezo utakaochezwa saa 10:00 jioni katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo.

JKU huo utakuwa ni mchezo wao wa pili wa kirafiki baada ya juzi Jumapili kucheza na Yanga huku wakifungwa 1-0 bao lililofungwa na Fiston Mayele.

Upande wa KMC huu ni mchezo wao wa kwanza wa kirafiki ikiwa ni sehemu ya maandalizi wakijiandaa na mchezo wao ujao dhidi wa Yanga utakaopigwa Oktoba 19 katika uwanja wa Majimaji Songea.

Mechi ya  Yanga na KMC imekuwa na vuta ni kuvute huku msimu uliopita mchezo wao wa kwanza walitoka sare 1-1 bao la KMC likifungwa na David Bryson na upande wa Yanga likifungwa na Yacouba Sogne.

Kwenye mechi ya pili Yanga ilishinda 2-1 bao la KMC likifungwa na Hassan Kabunda na mabao ya Yanga yalifungwa na Tuisila Kisinda (Penalti) kisha Waziri Junior alifunga bao la ushindi.