Kibu, Bocco waongeza mzuka Simba

WACHEZAJI wa Simba waliokuwa kwenye  timu ya Taifa Tanzania 'Taifa Stars' wamerejea katika mazoezi ya timu hiyo yanayoendelea kwenye uwanja wa Boko Veterani.

Wachezaji hao ni Mohamed Hussein 'Tshabalala', Israel Patrick Mwenda, Kennedy Juma, Kibu Denis na John Bocco.

Wachezaji hao wamerejea baada ya kutoka kwenye majukumu ya  Taifa Stars iliyokuwa inapambana na Benin Oktoba 10 kwenye kinyang'anyiro cha kuwania kufuzu fainali za Kombe la Dunia mwakani nchini Qatar.

Mwanaspoti limeshuhudia Kocha wa viungo wa timu hiyo Adel Zrane akiwapa mazoezi binafsi mabeki wa pembeni, Israel Mwenda na Mohamed Hussein 'Tshabalala', na wale wa timu ya vijana huku wengine wakiendelea na mazoezi ya pamoja.

Simba inajiandaa na mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF), dhidi ya Jwaneng Galaxy ya Botswana, mchezo unaotarajiwa kuchezwa Oktoba 17, nchini Botswana.