Fiston aanza kuaga Jangwani

Muktasari:

MSHAMBULIAJI Fiston Abdulrazaq ni kama ameanza kuaga Jangwani, baada ya kuweka bayana kwamba hataendelea Yanga mara baada ya mkataba wake wa miezi sita kumalizika, huku akijipigia debe Azam FC akisema ndio timu anayoipa nafasi kma ataamua kusalia nchini.

MSHAMBULIAJI Fiston Abdulrazaq ni kama ameanza kuaga Jangwani, baada ya kuweka bayana kwamba hataendelea Yanga mara baada ya mkataba wake wa miezi sita kumalizika, huku akijipigia debe Azam FC akisema ndio timu anayoipa nafasi kma ataamua kusalia nchini.

Fiston alitua Yanga katika dirisha dogo la msimu huu, lakini ameshindwa kuonyesha kiwango kwa kile kinachoelezwa ushindani wa namba kikosini, huku akiwa ameifungia timu hiyo bao moja tu katika Ligi Kuu Bara iliyopo ukingoni ikisaliwa na michezo ya mitano upande wa Yanga.

Akizungumza na Mwanaspoti katika mahojiano maalumu, Fiston alisema kwa sasa hafikirii kubaki Yanga hata kama angetakiwa kuongeza mkataba, kwa sababu ya mambo aliyokutana nayo Jangwani tangu alipojiunga nayo akitokea Esperance ya Tunisia.

“Nilikuja Yanga kucheza soka, sio kutembea mkataba wangu ulikuwa mfupi kwani nilitaka kuyaona mazingira kwanza, lakini kwa muda niliocheza sihitaji tena kuongeza mkataba,” alisema Fiston aliyeongeza;

“Mimi ni mchezaji, kazi yangu kucheza mpira sasa inapotokea mtu akanifanya nisicheze kwa mapenzi yake siwezi kuvumilia maisha haya nasema sitoweza kuongeza mkataba tena.”

Alisema katika timu kubwa zilizopo Bara yaani Simba, Yanga na Azam amebaini ni Azam pekee ndiyo inayoendeshwa kisasa kuliko nyingine.

“Azam ni timu haswa kwa jinsi ambayo inaishi na wachezaji wao, binafsi napenda sana lakini Yanga sio hivyo ikitokea nabakia Tanzania labda Azam tu ndiyo ninayoweza kuikubalia kubaki,” alisema Fiston na kuongeza;

“Cedric Kaze ndiye aliyenishawishi kuja kuichezea Yanga na kwa heshima yake nikaamua kuja nione na bora nilisaini muda mchache, sikuwa na habari kabisa za kucheza Afrika Mashariki, ila bahati mbaya wakati nakuja Kaze akaondoka, japo nilijiamini na kubaki hadi leo.”