Bocco, Kibu wang'aa dakika 45 za kwanza

NYOTA ya mshambuliaji John Bocco wa Simba imezidi kung’ara baada ya kutupia bao moja kati ya mawili yaliyofungwa kwenye kipindi cha kwanza cha mchezo wao dhidi ya Kagera Sugar.

Bocco amefunga bao la pili mfululizo baada ya kufunga bao moja kwenye mchezo uliopita Simba wakishinda 4-1 dhidi ya Ruvu Shooting.

Katika dakika za mwanzo timu zote zilianza kwa kupeleka mashambulizi kwa kuviziana ili kupata bao la kuongoza.

Dakika 5 Kagera walifanya shambulizi langoni kwa Simba baada ya Hassan Mwatelema kupiga shuti na kuungwa moja kwa moja na Hamis Kizza na mpira kutoka nje kidogo ya goli.

Simba dakika 13 ilipata bao la kuongoza baada ya Lary Bwalya kupiga krosi ya chinichini na Kibu Denis alionganisha mpira na kwenda wavuni.

Dakika 15 Simba ilifanya shambulizi lingine baada ya Kibu Denis kuchomoka na mpira na kupiga shuti akiwa ndani ya boksi la Kagera na kumgonga kipa, Said Kipao baada ya hapo ilitokea piga nikupige langoni kwa timu hiyo na kiungo Abdalah Seseme aliondoa hatari hiyo golini.

Kagera Sugar walilazimika kufanya mabadiliko dakika 27 baada ya beki Abdallah Mfuko kuumia na nafaszi yake aliingia Stephen Duah.

Dakika 28 beki wa Kagera Sugar alichomoka na mpira na kwenda spidi langoni kwa Simba na kupiga pasi kwa Hamis Kizza ambaye alipiga pasi kwa Ally Idd ambaye alikosa utulivu baada ya kuubutua mpira.

Dakika 30 Simba ilipata bao baada ya Lary Bwalya kupiga pasi kwa John Bocco ambaye alikimbia na mpira na kuingia ndani ya boksi kisha aliupiga mpira na kwenda wavuni moja kwa moja.

Kiungo Larry Bwalya alionekana kuwa katika kiwango kizuri akisambaza mipira kwa haraka kwenda langoni kwa Kagera Sugar.