Biashara: Waleteni hao simba

Muktasari:

BAADA ya kumalizana jana na Yanga katika mechi ya Ngao ya Jamii, kikosi cha Simba kitasafiri kuelekea Musoma Mara kucheza mechi ya kwanza ya Ligi Kuu kwa msimu wa 2021/2022 dhidi ya Biashara United ambao wamesema wamejiandaa kwa vita dhidi ya watetezi hao na wawakilishi wenzao wa CAF.

BAADA ya kumalizana jana na Yanga katika mechi ya Ngao ya Jamii, kikosi cha Simba kitasafiri kuelekea Musoma Mara kucheza mechi ya kwanza ya Ligi Kuu kwa msimu wa 2021/2022 dhidi ya Biashara United ambao wamesema wamejiandaa kwa vita dhidi ya watetezi hao na wawakilishi wenzao wa CAF.

Kikosi cha Biashara tayari kipo mjini Musoma mara baada ya kumalizana na FC Dikhil ya Djibouti walioing’oa katika Kombe la Shirikisho Afrika kwa jumla ya mabao 3-0 na sasa wanaisubiri Simba watakaovaana na keshokutwa, huku Kocha Patrick Odhiambo akifunguka wapo kamili gado.

Kocha huyo Mkenya alisema hahofii chochote katika mechi ya kwanza ya ligi dhidi ya Simba, licha ya kukiri mechi haitakuwa rahisi.

“Simba ni timu nzuri na kubwa hapa nchini lakini hiyo sio sababu ya kutudhoofisha kuelekea mechi ya kwanza ya ligi. Kikosi changu kipo kwenye hali na morali nzuri kuelekea mchezo huo. Tumejipanga kushinda mechi hiyo ambayo tutakuwa nyumbani,” alisema Odhiambo na kuongeza;

“Msimu huu tumepanga kufanya vizuri zaidi ya msimu uliopita hivyo tunahitaji kushinda mechi ya kwanza ili kuanza vizuri msimu,” alisema.

Mara ya mwisho timu hizo mbili kukutana kwenye mechi ya ligi ilikuwa Februari 12, kwenye Uwanja wa Karume, Musoma na Simba kushinda bao 1-0 lililofungwa na Bernard Morrison dakika ya 22 ya mchezo.