Barbara: Tumekuja kushinda

Dakika chache baada ya Simba kuwasili mkoani Kigoma kwa maandalizi ya mchezo wa fainali ya kombe la Azam (ASFC) dhidi ya watani zao Yanga, Ofisa Mtendaji Mkuu wa timu hiyo Barbara Gonzalez amefunguka kuwa wamekuja kushinda mechi hiyo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari nje ya uwanja wa ndege Kigoma, Barbara ameeleza mipango yao na kusisitiza kuwa wamejipanga kushinda mechi hiyo na kuwa mabingwa wa ASFC  kwa mara ya pili mfululizo.

“Tumefika Kigoma salama na kilichotuleta ni kutafuta ushindi tu.

Wachezaji wetu wako vizuri na wanalitambua hilo, tumeona namna Mashabiki wetu walivyotupokea kwa wingi wakiwa na furaha hivyo tutapambana kushinda ili kuwaheshimisha,” amesema Barbara.

Tayari timu zote mbili zipo mkoani Kigoma ambapo Yanga waliwasili Asubuhi na kuwawahi Simba waliowasili jioni ya leo.

Mtanange huo wa fainali umepangwa kupigwa Jumapili ya Julai 25, kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika Kigoma.