Sakho avuliwa jezi fasta, Phiri atajwa

STRAIKA wa zamani wa Simba na Taifa Stars, Emmanuel Gabriel ‘Batgol’, amekiangalia kikosi cha Msimbazi na kusema namba ya jezi aliyokuwa anaitumia enzi zake inayovaliwa kwa sasa na Pape Ousmane Sakho ni kubwa kwa mchezaji huyo na kutaka apewe Moses Phiri na kutoa sababu za hatua hiyo.

Akizungumza na Mwanaspoti, Gabriel aliyeibuliwa na Nazareth Njombe kabla ya kudakwa na Simba, alisema Sakho hastahili kuvaa jezi namba 10 kwa vile sio mchezaji hatari bali ni mchachari, na kutaka apewe Phiri mwenye mabao manne kwa sasa katika Ligi Kuu Bara na mawili michuano ya CAF.

Batgol alisema jezi namba 7, 9 na 10 huvaliwa na wachezaji hatari na sio machachari kama ilivyokuwa kwa Sakho, hivyo alisema hakuna ulazima wa Msenegal huyo kuendelea kuitumia na badala yake apewe Phiri anayeonekana ana makali zaidi.

“Unajua Sakho kabla hajapewa Tuzo ya Bao Bora Afrika zinazotolewa na CAF angalau alikuwa anaonyesha kiwango kizuri ingawa napo haikuwa sana, sasa hivi ndo amekuwa machachari zaidi ya mwanzo, hana msaada kwa timu, anacheza na jukwaa badala ya kuisaidia timu, sisi tunataka mafanikio ya timu sio machachari yake.

“Ninaomba jezi yangu namba 10 ithaminiwe kama nilivyoithamini wakati nacheza, zamani tulijitoa kwa ajili ya timu, hivyo ningependa jezi hiyo apewe Phiri, unamuona kabisa upambanaji wake na hachezi na jukwaa na anafunga, Sakho atafutiwe jezi za wachezaji machachari. Hadi sasa Sakho hajafunga bao Ligi Kuu.

“Nafahamu kila mchezaji anakuwa na chaguo lake la namba kwa namna anavyoona yeye, lakini jezi namba 7, 9 na 10 huwavaliwa na wachezaji hatari na sio machachari,” alisema Gabriel na kuongeza;

“Hata Clatous Chama alitakiwa avae jezi namba 7, ni mchezaji hatari anajitoa kwa ajili ya timu, ingawa namba 9 mara nyingi hukimbiwa na walioivaa miaka ya karibuni hakuna walichokifanya,” alisema.

Kwa upande wa jezi namba 9 kwa sasa haina mtu ndani ya Simba na kwa miaka ya karibuni ilivaliwa na Laudit Mavugo (Burundi), Frederick Blagnon (Ivory Coast), Wilker da Silva (Brazil), Betram Mwombeki.

Hata hivyo, mastaa hao walishindwa kuitendea haki jezi hiyo kutokana na viwango vyao kutokuwa bora ndani ya Simba.

“Sijui kwanini wanaiogopa hiyo namba maana haijavaliwa muda mrefu sana na waliowahi kuvaa hawakuitendea haki kama ilivyokuwa enzi zetu kwa wale wakongwe walioivaa jezi namba tisa,” alisema Gabriel.

Jezi hiyo, iliwahi kuvaliwa na wakongwe wa Simba kama Zamoyoni Mogela, Marehemu Edward Chumila ambao wote walikuwa washambuliaji akiwemo pia beki George Masatu.