Mnigeria Simba mambo freshi

KIUNGO wa Coastal Union aliyefunga penalti pekee ya timu hiyo wakati wakifungwa 4-1 na Yanga, Victor Akpan ameanza kuaga mashabiki na wachezaji wenzake akijiandaa kutua Msimbazi kwa msimu mpya wa mashindano.

Akpan aliyemwaga chozi wakati timu yake ikishindwa kubeba taji ya ASFC licha ya kuikomalia Yanga kwa dakika 120 ikitoka sare ya 3-3 na kupasuka kwenye matuta, alisema kilichomliza ni kuona wameshindwa kuibwaga Yanga waliyokuwa wameshaizidi ujanja mapema.

Akizungumza na Mwanaspoti, Akpan ambaye muda wowote atamwaga wino Msimbazi na kutambulishwa rasmi kwa msimu ujao alisema aliumia mno kupoteza mechi hiyo ya juzi ndio maana alimwaga chozi kabla ya kuwaaga wenzake na mashabiki kwa hatakuwa nao msimu ujao.

“Nilijikuta nalia kwa vile ni mchezo wangu wa mwisho kwenye timu, nilitamani tupate matokeo niache kumbukumbu, nimeshindwa kufikia malengo sijaacha kumbukumbu nzuri kwao nikajikuta nakutana na maumivu makali, ila nawapenda sana mashabiki wa Coastal, wachezaji wenzangu na benchi la ufundi nawatakia kila lakheri msimu ujao.”

Akpan akizungumzia ni wapi anaenda baada ya kuwaaga Coastal alisema sio wakati sahihi wa kuweka wazi hilo muda ukifika kila mmoja atafahamu msimu ujao atacheza wapi, licha ya ukweli Mwanaspoti linafahamu ameshazungumza na Simba na kilichobaki ni kusaini mkataba.