Fei Toto kumbe hajabahatisha

Fei Toto kumbe hajabahatisha

MFUNGAJI wa bao la kusawazisha la Taifa Stars dhidi ya Tunisia, Kiungo Feisal Salum ‘Fei Toto’ amelifungukia bao lake na kudai, alikuwa amejiandaa kabla ya kufumua shuti kwa namna alivyouona mpira.

Fei Toto anayekipiga Yanga, aliyeingizwa dakika 10 kabla ya mapumziko kuchukua nafasi ya Himid Mao, alifunga bao hilo kwa kufyatua shuti nje ya 18 na kwenda moja kwa moja wavuni na kuwapa ahueni mashabiki waliokuwa wanyonge baada ya kutanguliwa na wageni wao mapema.

Akizungumza na Mwanaspoti, Fei alisema baada ya nahodha wake John Bocco kuutuliza mpira ule alimuomba amuachie na hapo ndipo alipopiga shuti na kwenda moja kwa moja wavuni.

“Alipotuliza Bocco nilimuambia kapteni miee, hapo nikaangalia mpira nikaona upo sawa ndio maana nikapiga shuti, muda mwingine ni kama na-risk kwani naweza kufunga au kukosa lakini nashukuru nilifunga,” alisema Fei Toto, aliyeingia na kuibadilisha timu nzima ya Stars na kupata sare hiyo dhidi ya Tunisia.

___________________________________________________

THOMAS NG’ITU