KWAKO KASHASHA: Mastraika hawa nawakubali Ligi Kuu

KATIKA kolamu zilizopita, tumezungumzia walinzi, viungo wa pembeni na viungo wa kati ambao wameonekana kufanya vyema katika Ligi Kuu Bara msimu huu, leo tunatazama upande wa mshambuliaji namba moja ama centre forward au central striker.

Katika soka, kazi ya mwisho ni mpira kuingia wavuni baada ya kuwa umetembea umbali wa mita 90 au 120 kwa urefu na upana wa mita 45 hadi 90 kulingana na vipimo vya uwanja husika

Fikiria mpira umekimbia umbali wote lakini unatakiwa uingie katikati ya nguzo na nguzo na mtambaa panya wa goli ambalo lina urefu wa mita takribani saba kutoka mwamba mmoja hadi mwingine na kimo cha Mita 2.44.

Kwa hiyo unahamisha mpira kutoka mita 67 hadi sabini uingie katika goli lenye mita 7. Wakati huo hauko peke yako kuna kipa walinzi na viungo hivyo sio jambo rahisi. Hawa wamekuwa wakilaumiwa mara kwa mara pale wanapokosa bao lakini sio kazi nyepesi kuweka mpira kambani.

Katika ordha ya washambuliaji ambao wanaonekana wamefanya vizuri msimu huu, wa kwanza ni John Bocco. Amekuwa na msimu mzuri katika timu ya Simba na taifa. kaonyesha uwezo wa kufunga mabao.

Ana discipline ya kiufundi, ana kimo kizuri na uwezo wa kutumia kimo. Anaweza kutawala mpira.

Sifa nyingine ni pale anapokuwa katika nafasi ya kufunga atafunga na pale atakapokuwa hayuko katika nafasi atatoa pasi.

Bocco ana sifa nyingine ya discipline. Forward utakutana na harassment ya mabeki, utakuta kuna matumizi makubwa ya nguvu dhidi yake lakini anaweza kujidhibiti hayuko emotional.

Ndo maana ameweza kuwa nahodha. Usipokuwa mvumilivu kama mshambuliaji unaweza kujikuta ukicheza kwa muda mchache

Sifa nyingine anaweza kufunga mipira ya kuunganisha ile ambayo haijatulia. Ana target anapiga kwenye shabaha. Anajiweza na amekamilika. Akipona akarudi unaona mchango wake kwenye timu.

Straika mwingine ni Prince Dube. Anacheza kama false namba nine lakini anafanya majukumu kama mshambuliaji wa mwisho. Ni clinical finisher na anaweza kufosi bao.

Moto wake sio mdogo kwa sababu namna anavyojiweka kwenye position. Ni mtulivu, mpole na anafocus kwenye goli na anajua kusoma mchezo

Ameweza kucheza na washambuliaji wote. Ni mwepesi wa kucheza na mchezaji yeyote yule anayepangwa naye. Anatumia miguu yote miwili katika kufunga.

Kitu kingine ni mchezaji ambaye anaonekana yuko ambitious. Muda wowote anataka acheze. Nyingine hana tabia ya kugombana na waamuzi au wachezaji wa timu pinzani

Ameisaidia timu yake ya Azam kupata mabao ya kutosha akitokea upande wa kulia na kushoto.

Mshambuliaji mwingine ni Chris Mugalu. Ana uwezo wa kuhold mipira, kutoa assists,, anakimbia, anaguard mipira na kupiga krosi

Pamoja na uwepo wa washambuliaji tishio katika timu hiyo, bado ameonekana kuwa mshambuliaji tegemeo kwa sababu ya hizo sifa zake. Hakati tamaa muda wote

Ukiondoa hao mwingine ni mchezaji wa Namungo anaitwa Stephen Sey. Ni mchezaji ambaye amekuwa msaada mkubwa japo timu yake haijafanya vizuri na kuna mwingine yupo Mbeya City anaitwa Kibu Denis.

Wote ni wapambanaji, wana tamaa ya goli, na ni wazuri kwenye pasi za mwisho. Wanakufunga kwa miguu na wanaweza kukufunga kwa vichwa.

Kwa ujumla wao ni mastraika ambao wanajua kujiposition vizuri. Mabao ambayo wanafunga yananifanya niwaweke katika orodha ya nyota ambao naona wamefanya vizuri msimu huu.

Kibu Denis ana safari ndefu lakini staili yake ya uchezaji ni ya utulivu mno katika final third. Kama ataendelea hivyo atakuwa msaada zaidi na zaidi. Hana woga na anaweza kupambana. Ana uwezo mkubwa wa dribble mpira, Ni aina ya wachezaji wachache wenye uwezo wa kusepa na kijiji katika Ligi Kuu ya Bara.


IMEANDIKWA NA ALEX KASHASHA