Vanessa avishwa pete ya uchumba

Penzi la mwanamuziki Vanessa Mdee na muigizaji wa Marekani mwenye asili ya Nigeria limezidi kunoga baada ya Rotimi kumvisha pete ya uchumba dada yetu usiku wa kuamkia leo Desemba 31.

Kupitia video iliyopostiwa kwenye ukurasa wa Instagram wa The Shade Room, anaonekana Rotimi akiwa amepiga goti, huku akimuomba Vanessa akubali kuvishwa pete hiyo, ambapo Vanessa alikubali huku akilia kwa furaha.

Baada ya video hiyo, pia ilichapishwa video nyingine ikiwaonyesha wawili hao na watu wao wa karibu wakipata chakula cha jioni kisha Vanessa alionyeshea pete vizuri zaidi kwa kuisogeza karibu na kamera.

Uhusiano wa wawili hao ulianza mwaka 2019 baada ya Vanessa kuachana na aliyekuwa mpenzi wake, mwanamuziki wa Tanzania, Jux.

Kwa sasa Vanessa ambaye mwezi Juni alitangaza kuachana na shuhuli za muziki anaishi Marekani pamoja na mwanume huyo na mara kadhaa amekaririwa akimsifia kuwa ni mwanaume aliyefanya aitambue thamani ya maisha yake.

Kwenye moja ya 'podcast' zake za Deep Dive with Vanessa, Vee Money alifunguka; "Rotimi amenifanya nijue thamani yangu. Kabla ya kukutana tulikuwa na maisha huko nyuma, lakini ni kama hayahesabiki tangu tumeanza haya maisha yetu mapya, hususan vitu hasi."

Rotimi ambaye jina lake kamili ni Olurotimi Akinosho, ni mwanamuziki na muigizaji. Anamiliki ngoma kali kama vile Meeting In My Bed na Love Somebody. Pia amecheza kwenye tamthilia maarufu ya Power na filamu ya Divergent.