Rose Ndauka aibukia kwenye Hiphop

Muktasari:

  • MSANII Rose Ndauka, amegeukia kuimba muziki wa hiphop, ikiwa ni katika kutumiza ndoto zake za kuwa muimbaji.

MSANII Rose Ndauka, amegeukia kuimba muziki wa hiphop, ikiwa ni katika kutumiza ndoto zake za kuwa muimbaji.


Akizungumza leo Alhamisi, Aprili 8,2021 na waandishi wa habari, alipokuwa akitambulisha wimbo wake wa Sijali, amesema ndoto za kuimba alikuwa nazo kabla ya kuanza uigizaji hivyo anafutahi kuzikamilisha kwa sasa.


Rose ambaye ni mama wa watoto wawili, amesema anaamini kwa kufanya hivyo pia atakuwa amewaonyesha upande wa pili mashabiki zake wanaomfuatilia katika uigizaji na kueleza kuwa hatawaangusha huku akiwaomba wampe sapoti kwa kuwa bila wao hawezi kusonga mbele katika hili.


"Nawaomba mashabiki zangu waliinikubali katika filamu hadi leo kuwa na umaarufu niliokuwa nao,wanisapoti pia kwenye  muziki wangu ili niendelee kuja na mambo mazuri na kuwa mmoja watu wenye mchango katika muziki wa Tanzania,amesema," amesema msanii huyo.


Wakati kuhusu matarajio yake katika muziki huo,amesema ni kuja kufanya kazi na wasanii wengine akiwemo Rosaree, Shilole na wengine waliomo katika muziki huo.


Kuhusu maneno ya kuwepo kwa ugumu katika muziki huo na hususani kwa wasanii wa kike, Rose amesema yeye haoni ugumu isipokuwa anaamini ni juhudi za msanii na sapoti kutoka kwa watu na ndio maana wengine wapo hadi leo.


"Hakuna cha ugumu katika kazi yeyote ni wewe tu kujiwekea mikakati ya namna gani ya kufanya kazi yako kwa ubora  na watu kukukubali na kukusapoti,ndio maana pia nimeomba sapoti kutoka kwa watu ili niwezi kutimiza adhma yangu hii ya kuielimisha jamii kupitia muziki pia" amesema.

Rose alipata umaarufu mwaka 2007   kupitia  filamu ya “Swahiba” aliyoigiza na wakali kama Jacob Steve na Single Mtambalike 'Rich'.

Baada ya filamu hiyo Rose aliweza kupata nafasi ya kuigiza katika filamu mbalimbali zikiwemo Mahabuba na Solemba na Deception aliyocheza na marehemu Steven Kanumba na Lost Adam.