JIDE: Mastaa wa nguo za mamilioni waongo

Muktasari:

MMESIKIA? Dada Mkuu Jide a.k.a Commando a.k.a Anaconda anafichua kuwa, wasanii wenye majina makubwa wanaojitapa kuwa wamevaa nguo za mamilioni wanapiga fiksi.

MMESIKIA? Dada Mkuu Jide a.k.a Commando a.k.a Anaconda anafichua kuwa, wasanii wenye majina makubwa wanaojitapa kuwa wamevaa nguo za mamilioni wanapiga fiksi.

Jide ameyasema hayo baada ya kuulizwa huwa anatumia shilingi ngapi katika kuvaa ambapo alieleza kuwa mara nyingi nguo zake ni za kawaida sana na pia hufuatwa na watu kutaka wamvalishe kwa lengo la kujitangaza.

“Jamani mimi navaa kawaida tu kama watu wengine, na ukiniona nimevaa nguo ya gharama kubwa jua kuna watu wamenivalisha,” alisema.

Mkali huyo wa kibao cha Ndi ndi ndi, alisema msanii anaweza akawa kaenda kwenye shughuli inayowakutanisha watu mbalimbalii, lakini kuanzia chini mpaka juu kuna wavalishaji tofauti wamesababisha kupendeza kwake.

Alisema hiyo ndio moja ya faida mtu ukishakuwa na jina, kwani wapo wanaovalishwa na kulipwa na wapo wanaovalishwa kwa lengo tu la kutangaza bidhaa ya mtu.

“Kuna mtu anakuvalisha halafu malipo yake wewe utaje tu nimevalishwa na fulani basi na hapo ndipo wasanii na mastaa wengi wanapoponeaga katika kuepuka gharama za kuvaa,” alisema Jide ambaye jina lake halisi ni Judith Wambura.

Staa huyo hivi karibuni amesherehekea miaka 20 ya kuwa kwenye gemu hii.