Harmonize kutumbuiza Singida Big Day

MSANII  nyota wa Bongo fleva Harmonize 'Konde Boy'  ametangazwa na timu ya Singida Big Stars kuwa atatumbuiza katika tamasha lao linaloitwa 'Singida Big Day' litakalofanyika Agosti 4 2022 katika Uwanja wa Liti (zamani Namfua).

Sherehe hizo ni maalumu kwa ajili ya kutambulisha kikosi kizima cha timu hiyo, jezi mpya za msimu na benchi nzima la ufundi huku kikichagizwa na mchezo wa kirafiki dhidi ya Zanaco ya Zambia.

Msanii huyo atatumbuiza katika tamasha hilo ikiwa ni siku chache baada ya kuwashangaza mashabiki zake kufuatia kumchangua mpenzi wake Kajala kuwa meneja wake mpya.

Aidha staa huyo ambaye anatamba na albamu zake kama Afro East na High School anasifika kwa kucheza aina za kipekee kwenye mziki wa amapiano.

Miongoni mwa ngoma zake kali zinazotamba kwa nyota huyo ni, Sandakalawe, Turn-Up, Deka, Bedroom, Never give up, Uno, Mama na Hujanikomoa.