Hamisa atoa neno picha za Diamond, Zari

WAKATI mapicha mapicha yanayomuonyesha msanii wa Bongo Fleva, Diamond Platnumz akijivinjari na watoto wake wawili aliozaa na mfanyabiashara wa Kiganda, Zari 'The Boss Lady', Tiffah na Nillan yakiendelea kusambaa kwenye mitandao ya kijamii hasa Instagram, mzazi mwenza mwingine wa Diamond, Hamissa Mobetto ameibuka na kueleza kuwa haumizwi na picha hizo.
Hamisa amefunguka hayo leo Jumanna Novemba 10, 2020 jijini Dar es Salaam, alipozungumza na Waandishi wa Habari wakati anasaini mkataba wa ubalozi wa kampuni ya kutengeneza taulo za kike za HQ.
“Sina comment kwenye maisha ya watu wengine, lakini kila kinachoendelea hakiniumizi na tena maisha yangu yako vizuri kama kawaida,” amesema Hamissa.
Hamisa na Diamond wamebarikiwa mtoto mmoja wa kiume anayeitwa Dylan (4), ambaye licha ya kwamba mara kadhaa kumekuwa na picha zinamuonyesha mtoto huyo akiwa na baba yake, lakini hazikuwahi kuwepo zinazowaonyesha katika ‘family moment’ yenye shangwe kama ilivyo kwa watoto wa Zari.
Tangu watoto hao waingie nchini kutoka Afrika Kusini wanapoishi na mama yao, wamepelekwa kuziona ofisini za chombo cha habari anachomiliki Diamond, pia kwenye kiwanda kinachozalisha soda ambacho Diamond ni balozi wa bidhaa hizo, vitu ambavyo Dylan hajawahi kufanyiwa.
Hamisa alipoulizwa kama anadhani Diamond ana ubaguzi kwa watoto aligoma kujibu, na hata alipolazimishwa alitoa jibu moja tu la “No comment.”
Mchezo uko hivi
Novemba 05 mwaka huu, Zari alitua nchini kwa ajili ya kuwaleta watoto hao ikiwa ni miaka miwili imepita tangu wakutane na baba yao.
Hata hivyo, licha ya Zari kudai kuwa ujio huo ni kwa ajili ya kuwaleta watoto wamuone baba yao, kumekuwa na tetesi za kwamba huenda amerudisha majeshi na labda hivi karibuni itawekwa wazi kuwa penzi lao limefufuka.