Dereck Chisora ashindwa kufurukuta kwa Joseph Parker

Muktasari:

Tangu kuanza ngumi, Parker amewahi kupigwa mara mbili, mwaka 2018 dhidi ya Dillian Whyte na Anthony Joshua, mapambano yote alichapwa kwa pointi na kushinda mapambano 29 (21 kwa KO).

Bondia namba 10 kwenye uzani wa juu, Dereck Chisora ameshindwa kufurukuta nyumbani na kuruhusu kipigo dhidi ya Joseph Parker katika pambano la uzani wa juu lililopigwa usiku wa kuamkia leo huko Manchester Arena, Uingereza.

Refarii, Steve Gray alimtangaza Parker raia wa New Zealand anayekamata namba tisa ya dunia kwenye uzani wa juu kuwa bingwa wa mabara wa dunia wa mkanda wa WBO kwa majaji 2-1.

Katika pambano hilo la raundi 12, jaji namba moja, Andrew Bell alitoa ushindi wa pointi 115-113 kwa Parker na jaji namba tatu, Grzegorz Molenda alimpa 116-111 na jaji namba mbili, Howard Foster alimpa ushindi wa pointi 115-113 Chisora.

Kabla ya pambano hilo, 1,105 alikuwa amempiku kwa nafasi moja Chisora ambaye ni bondia namba 10 duniani kwenye uzani wa juu kati ya mabondia 1,105, wote wawili wana nyota tano.

Katika nchi zao, Parker mwenye miaka 29 anayejiita kwa utani Lupesoliai La'auliolemalietoa ni bondia namba moja kati ya 24 wa uzani wa juu nchini New Zealand.

Chisora au War kama anavyopenda kujiita mwenye miaka 37 ni aliyezaliwa Mbare, Zimbabwe anakamata nafasi ya nne kati ya mabondia 42 wa uzani wa juu nchini Uingereza ambako sasa ana uraia wa nchi hiyo.