Basata yawaonya kiaina Harmonize na Rayvanny

Muktasari:

  • Unaweza kusema Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) limewaonya kiaina wasanii wa Bongofleva, Harmonize na Rayvanny.

Dar es Salaam. Unaweza kusema Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) limewaonya kiaina wasanii wa Bongofleva, Harmonize na Rayvanny.

Takribani siku tatu sasa wasanii hao wamekuwa wakirushiana vijembe mitandaoni  huku chanzo kikitajwa kuwa ni mwigizaji wa filamu, Kajala na mwanaye, Paula.

Leo Jumatano Aprili 14, 2021 baraza hilo limekemea mienendo na vitendo vya wasanii kulumbana na kutumia lugha zisizo na staha kwenye mitandao ya kijamii sambamba na kuonya usambazaji wa video zisizofaa unaofanywa na wasanii kwa lengo la kudhalilishana.

Taarifa iliyotolewa na kaimu katibu mtendaji wa baraza hilo, Matiko Mniko bila kuwataja wasanii hao inaeleza kuwa hawatasita kuchukua hatua kali kwa msanii atakayebainika kuendeleza vitendo hivyo.

Mniko amesema vitendo hivyo vinarudisha nyuma juhudi za Serikali za kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa wasanii na wadau.

Amesema sekta ya sanaa inahitaji juhudi za wasanii na kuongeza ubunifu ili kunyakua tuzo kubwa za kimataifa  kuliko kudhani ‘kiki’ za kuchafuana ndio msingi wa mafanikio.