Babu Tale aomba msaada wa wanasaikolojia

Muktasari:

  • Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Hamisi Taletale maarufu Babu Tale, amesema anahitaji kukutana na mwanasaikolojia kutokana na kipindi anachokipitia.

Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Hamis Taletale maarufu Babu Tale, amesema anahitaji kukutana na mwanasaikolojia kutokana na kipindi anachokipitia kwa sasa baada ya kumpoteza mke wake.


Mke wa Tale aliyekuwa akifahamika kwa jina la Shammy, alifariki Juni, 2020 na kumwachia watoto watatu.


Kupitia ukurasa wake kwenye mtandoa wa Instagram leo Ijumaa Julai 16, 2021, Tale ambaye pia ni meneja wa msanii Diamond Platnumz, ameandika kuwa hajawahi kutamani kukutana na mwanasaikojia ila kwa sasa anahitaji maana hali yake sio nzuri kwenye hiki anachopitia.


“Kuna vitu omba visikukute katika maisha yako. Usiombe uondokewe na mke au mume. Mimi napitia maisha magumu sana kila ukiona unakaribia kukaa sawa kumbe unajiona bado maumivu hayaishi."

Babu Tale na mkewe enzi za uhai wake.


“Maana leo nina siku ya tatu naamka tisa usiku vilio na maumivu yasioisha. Sijawahi kutamani kukutana na mwana saikojia ila kwa sasa nahitaji kwakweli maana hali yangu sio nzuri kwenye hiki ninachopitia.


“Namkumbuka sana mke wangu. Mungu aendelee kukulaza mahala pema Mama TT,”ameandika Babu Tale.