Baba Levo apigwa faini ya Sh1 milioni na Basata

Muktasari:

Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) limemtoza faini Msanii wa vichekesho na muziki, Clayton Chipando maarufu baba Levo ya Sh1 milioni kwa kosa la kusambaza wimbo bila kuupeleka kuhakikiwa kwenye baraza hilo.

Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) limemtoza faini Msanii wa vichekesho na muziki, Clayton Chipando maarufu baba Levo ya Sh1 milioni kwa kosa la kusambaza wimbo bila kuupeleka kuhakikiwa kwenye baraza hilo.

Baba Levo ameyasema hayo leo Ijumaa Aprili 16,2021  alipozungumza na waandishi wa wahabari na kuweka wazi kile alichoitiwa na baraza hilo jana na pamoja na kuhojiwa kwake na Jeshi la Polisi.

Pamoja na mambo mengine alizungumzia kwa Basata amesema kubwa waliomuitia ni hilo la kurusha wimbo bila kuhakikiwa na kueleza tayari leo amepokea barua ya kutoka kwao ya kupigwa faini ya Sh1 milioni.

"Jana kama mlivyoniona pale Basata niliitwa lakini kubwa ni kuhusu wimbo wangu ambao haukupitia taratibu katika kuutoa na tayari nimepokea barua ya onyo na kupigwa faini," amesema Baba Levo.

Mbali ya faini pia alitumia nafasi hiyo kuomba radhi kwa umma wa watanzania kwa yeyote aliyekerekwa na wimbo huo kwa namna moja au nyingine

Wakati kwa upande wa kuitwa Polisi, amesema alichoitiwa ni kudaiwa kusambaza picha za utupu zinazodaiwa kuwa ni za msanii Harmonize.

Hata hivyo ameeleza kuwa anasubiri kesi hiyo ifike mahakamani ili aweze kudai fidia ya Sh6 bilioni kwa kuwa anaamini hajahusika na hayuko tayari kumuona mtu akitumia jina lake kutafuta kick.