Ali Choki akanusha kuwa Marioo

Wakati kulikuwa na tetesi kwamba kupotea kimuziki kwa msanii maarufu wa muziki wa dansi, Ali Choki, kulitokana na mkewe kufariki, mwenyewe aweka hadharani kilichomtokea.

Choki ameyazungumza hayo leo Alhamisi Novemba 12, 2020 katika mahojiano na Mwanaspoti, alipotembelea ofisi za kampuni ya Mwananchi zilizopo Tabata Relini, jijini Dar es Salaam.

Msanii huyo ambaye aliwahi kutesa na vibao mbalimbali ikiwemo Chuki binafsi, Aminata na vingine vingi, katika ziara hiyo amefunguka mambo mengi ikiwemo sakata la kunyang’anywa mali na ndugu wa mke wake mama Shuu, aliyefariki mwaka 2014.

Choki alisema mama huyo ambaye alikuwa vizuri kimaisha, walichuma naye baadhi ya mali ikiwemo nyumba waliokuwa wanaishi naye maeneo ya Kigamboni.

Hata hivyo alisema baada ya kufariki, ndugu walionekana kuitolea nyumba hiyo macho ambayo thamani yake ni zaidi ya Sh500 milioni.

“Sikutaka kuingia nao katika malumbano kuhusu mali tulizochuma na ndugu yao, hivyo niliamua kuchana nayo na kwenda kuanza maisha yangu mapya kwa kuwa mimi mwananume na mali zinatafutwa na hata katika maisha ya kifamilia niliyotoka hatukuwa tunamiliki hata baisikeli, sasa kwa nini nihatarishe uhai wangu kwa vitu ambavyo vinatafutwa,” ameeleza Choki.

Alisema ni kutokana na mgogoro huo alichoondoka nacho ni vyombo vyake vya muziki vilivyokuwa vimejaa fuso nzima na gari zake mbili ambapo hata hivyo nyumba hiyo alikuja kukabidhiwa mtoto wa marehemu baadaye.

Wakati kuhusu stori za kulelewa na marehemu, Choki amesema hazina ukweli wowote kwani wakati wanakutana naye tayari alikuwa na jina lake mjini na hata leo maisha kwake ya utafutaji bado yanaendelea.

“Huwezi kuwazuia watu kuzungumzia yale wanayodhani kwao ni sahihi japokuwa ukweli wa maisha tunaujua sisi wenyewe. Mimi wakati najuana na mama Shuu nilikuwa tayari nina jina langu mjini nina maisha yangu, tulichofanya ni kuunganisha nguvu na kuendeleza muziki wangu, lakini sio kulelewa kama wanavyosema walimwengu,” amebainisha.