Yaani kwio! cheki vichwa 10 zenye singeli yao

Muktasari:

Mwanaspoti linakuletea wasanii 10 ambao wanatamba kwenye na kwa kiasi kikubwa wameubeba muziki huo na kuuweka katika ramani ya dunia. Hata huko mitaani mambo ni mazito kwelikweli kwani, kila ukipita unasikia midundo ya singeli tu.

KAMA bado unadhani kuwa muziki wa singeli ni wa kiswazi basi pole yako buana. Jamaa kwa sasa wanazidi kupasua anga na wameufikisha muziki huo kwenye anga za kimataifa.

Ndio, singeli sasa imetua kwa Donald Trump hukooo Marekani ambapo, Mtayarishaji na supastaa Swiz Beats na mkewe Alicia Keys huwaelezi kitu.

Hivi karibuni video ya Alicia na Beats ndio imebamba kinoma wakionekana wakicheza ngoma mpya ya Wanga ya Meja Kunta aliyomshirikisha Lava Lava.

Ngoma hiyo imepenya kutokana na namna ambavyo mashairi yake, midundo na sauti zenye vionjo vitamu za wasanii hao ambao, kwa sasa ndio habari ya mujini.

Katika kuonyesha kuwa singeli imekuwa habari ya mjini hata mastaa wa Bongo Flava nao wameingia kweye anga hizo wakifanya ngoma na wasanii wa singeli na mwisho wa yote huishia kubamba kinoma.

Mwanaspoti linakuletea wasanii 10 ambao wanatamba kwenye na kwa kiasi kikubwa wameubeba muziki huo na kuuweka katika ramani ya dunia. Hata huko mitaani mambo ni mazito kwelikweli kwani, kila ukipita unasikia midundo ya singeli tu.

MEJA KUNTA

Mamu mamu, nisamehee mke wangu jana nilikosa mke wangu, ooh Mamu Aaah Aaah Aaaah Aaah Aaaa

Ooooh Mamu Oooh Mamu Ooh Mamuuuu

Ngoma hii ilibamba nab ado inaendelea kubamba na kwa kiasi kikubwa ilimtambulisha Meja Kunta kwenye game ya singeli. Katika ngoma hii Meja Kunta alimshirikisha staa wa Bongo Fleva, Mr Blue a,k,a Kabaysa na kupenya kwenye masikio ya mashabiki.

Lakini, wakati hata bado haijapoa kwanza ikasikika kwamba, Meja Kunta amepata ajali na kupoteza maisha. Huku na kule wafukunyufu wakazinyaka kuwa hiyo ni kiki na dogo alikuwa mbioni kuachia ngoma mpya na mara paap ikashuka ‘Wanga’ ambao hadi Alicia Keys na Beats wameikubali.

Ujio wake umeongeza kitu katika mziki wa Singeli na kuwaaminisha watu kwamba, sio mziki wa kiuni kama baadhi ya watu wanavyoamini.

MZEE WA BWAX

Unaringa unaringa una nini weweeee

Unaringa unaringa una nini maamaaa

Unajishongodoa, unajishauaaaa

Umenunua dela, umekopa vikobaaaaaa

Kutwa kujichubua, mashauzi yamezidi

kutwa kushinda kwa jirani, kuazima mawigiii

Hiki ni kionjo ambacho kipo kwenye ngoma yake ya ‘Unaringa Nini’ Mzee wa Bwax anasifika kwa mashairi yenye maana na kugusa jamiii licha ya kuwa huwa anagusa sana upande wa wanawake.

Bwax hivi karibuni amekuwa maarufu hasa ngoma zake zikipendwa na wachezaji wa mpira kama Ibrahim Ajibu na Said Ndemla.

Wimbo wake mkubwa ambao ni kama uliiteka Bongo ni ule wa ‘Kisimu Changu’ ni wimbo unaobamba rika zote na kukubalika kinoma.

DULLA MAKABIKLA

Achana na ngoma zake za nyuma, kwa sasa anatamba na Ningekuwa Demu, akiwa ametumia sanaa kuwakilisha ujumbe kwenye jamii. Siku kitu cha kushtua sana kwa wanamuziki kwani hata Beyonce Knowles aliwahi kuandika na ngoma ya ‘If where i am boy’.

Hata hivyo, wabongo hawakumuelewa kabisa Dulla kwani, waliona kama kitu Fulani tofauti kidogo kwenye jamii.

Makabila zamani aliwahi kuachia ngoma kama Ujaulamba, Dua na Waongo ambazo pia zilibamba kinoma.

MAN FONGO

Nasikia hainaga ushemeji, tunakulaga

Wanangu zamu ya nani leo, zamu ya Man Fongo

Zamu yako itakuja kesho usikonde baharia wangu

Ni bonge la ngoma ambalo aliwahi kulifanya na likamuweka katika ramani ya singeli mpaka leo akiendelea kuachia ngoma zingine zikidumu.

Man Fongo ameweza kukaa katika mstari huku akichia ngoma zenye mvuto kwa wapenzi wa singeli mfululizo kama vile ‘Yeye’.

SHOLO MWAMBA

Kama una geto mwanangu onyesha funguo

We kama una geto mwamba onyesha funguo

Masela tuna mageto, we mwamba nina geto langu

Hii ni nyimbo ambayo masela wote wakiwa wapo katika singeli ikipigwa utaona wananyanyua funguo zao wakizungusha.

Uliteka hisia za masela wengi ambao wanamiliki mageto yao kiufupi jamaa aliweza kuwateka mashabiki wa singeli hali iliyomfanya mpaka afanye ngoma na Prof Jay.

PROF JAY

Usishangae kuona nikimuweka humu kwenye wasanii wa Singeli, jamaa ni kama alishtuka

hivi kufanya ngoma na Sholo Mwamba kwani kipindi hiki alikuwa anatamba na yeye ndio

akaachia zake ngoma ‘Kazikazi’ iliweza kutamba vilivyo.

Baada ya kuachia ngoma hii mchizi wala hakuendelea na singeli bali aligeukia mishe zake za Ubunge kuhakikisha mambo yanaenda sawa.

MSAGA SUMU

Kumbe unanitega Shemeji, unanitesa mamaa weee

Unataka nini shemeji eeh, unanitega mama weeeeeee

Ni ngoma ambayo alizungumzia namna ambavyo anategwa na shemeji yake kwa namna ambavyo vituko alivyokuwa anamfanyia, wimbo ulipenya na kukubalika.

Baada ya hapo alikuja kuachia ngoma kali kama mwanaume Mashine, Mwache Adange na zote zikiwa kali kupitiliza na kuendelea kubaki na mashabiki wake.

Licha ya kwamba wasanii wengine wa mziki huo wanakuja lakini yeye ameendelea kusalia katika mziki huu kwa kiwango hiko kutokana na mashairi yake ambavyo anayatunga.

SNURA

Ni mdada mrembo lakini naye baada ya kutoa ngoma ya Chura baadaye aliamua kuingia

kwenye singeli na kuachia ngoma ya ‘Zungusha’.

Wimbo huu licha ya kwamba ulifanywa na mwanadada, uliweza kupendwa na watu wa singeli kutokana na video yenyewe ya kuchezeka pamoja na mdundo uliotengenezwa.

PAM D

Ukimuona wala hauwezi kutarajia kutokana na urembo wake huyu mwanadada lakini aliamua kuingia katika singeli tena kwa kuimba na mkali wao Msaga Sumu.

Kuingia kwa mdada mzuri kama Pam D kunafanya zaidi mziki wa Singeli kuzidi kulainika kutoka kule ulipokuwa unaaminika kwamba ni uhuni na kuwa mziki wa watu wote na kusikilizwa sehemu yoyote ile.

HARMONIZE

Mwambieni dada yenu hajanikomoa,eti badala ya kujenga unabomoa.

Huu ni wimbo ambao unatamba hivi sasa kwa namna ambavyo jamaa ameweza kubadilika kutoka kwenye kubana pua mpaka kwenye ngoma za Singeli.

Kikubwa zaidi ni kwamba Hermonize ameweza kabisa kufanya kama vile ambavyo wenzake wamekuwa wakifanya katika ngoma hizi.

Wengi walikuwa wanataka kusikia namna ambavyo amebadilika na kiukweli hajawaangusha kwani kafanya kile ambacho walikuwa hawatarajii.