Vichambo vya Insta vyamuibua Malaika

Muktasari:

  • Pia, ikawa mbaya tena kwa msanii wa filamu, Wastara Juma ambaye alikutana na hali kama hiyo kutoka kwa mwanadada huyo, jambo ambalo liliibua hisia tofauti.

MTANDAO wa Instagramu kwa sasa ndio umekuwa kama mahakama unaambiwa kwani, mtu akizingua tu anapelekwa huko kuchambwa. Wiki iliyopita hali ilikuwa mbaya kwa dada wa Diamond, Esma Platnumz ambaye alikutana na vichambo kutoka kwa Mange Kimambi.

Pia, ikawa mbaya tena kwa msanii wa filamu, Wastara Juma ambaye alikutana na hali kama hiyo kutoka kwa mwanadada huyo, jambo ambalo liliibua hisia tofauti.

Hata hivyo, vichambo kwenye mitandao ya kijamii vikamuibua staa wa kike wa Bongo Flava, Malaika ambaye ameiasa jamii hasa wale waliopata elimu, kuitumia vyema mitandao ili kupiga pesa na kuhamasisha umoja.

Pia, ametaka elimu hiyo ya matumizi bora ya mitandao ya kijamii ili kuokoa kizazi cha sasa na vile vijavyo kuepukana na chuki na migogoro inayoweza kupoteza hadhi ya mtu mbele ya jamii.

“Tunaweza fundisha jamii yetu kwa njia tofauti pindi tunapotumia mitandao ya kijamii na kujenga kizazi bora, tunapofundisha ubaya tunajenga kizazi cha chuki na kuondoa thamani ya utu katika jamii, hivyo elimu inatakiwa katika hili,” alisema Malaika.