Shonza abeba msalaba wa Chid Benz

Muktasari:

Chid Benz amekuwa bora mara kwa mara katika mziki wa kufokafoka lakini kujiingiza katika madawa ya kulevya kulimrudisha nyuma.

NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini, Juliana Shonza ameamua kumpa sapoti msanii wa muziki wa Hip Hop, Rashid Makwiro 'Chid Benz'.

Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram, Shonza aliweka picha akiwa amekaa na msanii huyo na kuonyesha kufurahia ugeni huo na kuahidi kumsapoti katika muziki wake.

"Hiki chuma kipo imara zaidi ya jana nilifurahi jana kutembelewa na msanii nguli wa muziki wa Bongo Fleva ofisini kwangu Dodoma, ikiwa ni ahadi yake aliyoniahidi nilipokutana naye siku ya uzinduzi wa albamu Lulu Divaz," aliandika.

Shonza alimsifia msanii kwamba ana uelewa mpana wa sanaa na ukikaa naye ana uwezo wa kuongea mwenyewe bila kukupa nafasi hata ya saa mbili.

"Amenieleza mikakati  yake aliyonayo ya kurudi kwa kishindo kwenye muziki ikiwemo ujio wa nyimbo yake itakayotoka Jumatatu iitwayo 'Beatiful', kubwa ameniambia hivi sasa anataka kufanya kazi zake za sanaa kwa kusajili Sokota,".

Aliongeza kwa kuandika msanii huyu amewashukuru sana mashabiki wake kuendelea kuwa na imani naye wasanii wenzie na wadau wa muziki kumuamini na kumualika kwenye shoo mbalimbali licha ya changamoto alizopitia.

"Kwa upande wangu kama mlezi wa sanaa Tanzania nimeahidi kumpa ushirikiano wa kutosha katika kazi zake ili kumuepusha kurudia mambo yanayoweza kuhatarisha maisha yake,".