Rosaree afichua ile ‘Only You’

ONLY YOU’ ukiwa kati ya nyimbo zilizoachiwa mwezi huu, msanii wa bongoflevasit Rosary Robert maarufu ‘Rosaree’ afichua siri hadi kujikuta akishirikishwa kuuimba.

Rosaree ameshirikishwa na msanii anayefanya vizuri katika muziki wa dansi, Christan Bella, ikiwa ni mara ya kwanza kumuona msanii huyo aliyejikita katika aina ya muziki wa kufokafoka akishirikiana na wasanii wa dansi.

Akieleza namna alivyokutana na Bella hadi kujikuta anafanya naye ngoma hiyo, msanii huyo alisema ni baada ya siku moja Bella akiwa anahojiwa katika moja ya kituo cha redio kusema angetamani siku moja kufanya kazi naye.

“Kuna siku kaka yangu Bella alionyesha matamanio yake ya kutaka kufanya

kazi na mimi, na baada ya mahojiano hayo alinitumia ujumbe mfupi kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram na tukachati mengi hadi kufika hatua ya kupeana namba na kuja na mpango huo wa kutengeneza wimbo huo wa ‘Only You’,” alisema Rosaree.

Akizungumzia kuhusu mapokeo yake, Rosaree alisema ni mazuri na kuongeza kuwa anashukuru namna mashabiki ambavyo wamewapokea.

Wakati kuhusu kama aliwahi kuwaza kufanya kazi na msanii wa dansi, alisema hakutegenmea japokuwa kwake ni nafasi nzuri kwani amekuwa akipenda kuwa msanii wa kubadilika.

Akimzunguzia Christiana Bella kuwa ni mtu wa aina gani kwa muda mfupi waliofahamiana kufanya naye kazi, alisema ni mtu mcheshi, anapenda watu na anapenda amani na kufanya kazi kwa bidii.

Rosaree ameshaachia vibao mbalimbali ikiwemo Banjuka, Nguvu za Kiume na Sukuma Ndinga.