Riyama Ally amkabidhi msiba wake Steve Nyerere

Muktasari:

  • Shughuli za msiba wa Ruge Mutahaba umewakutanisha kwa mara ya kwanza Steve Nyerere na Ommy Dimpoz.

Dar es Salaam. Mcheza filamu Riyama Ally amemwambia mwigizaji mwenzake Steve Nyerere siku akifariki aubebe msiba wake.
Riyama ametoa kauli hiyo leo katika msiba wa Ruge Mutahaba baada ya kuona Steve Nyerere na Ommy Dimpoz wakipiga stori za matani kama hakuna kilichotokea kati yao.
Hivi karibuni Steve Nyerere alinukuliwa katika mitandao ya kijamii akisema Dimpoz hatoimba tena baada ya kufanyiwa upasuaji wa koo, lakini mwanamuziki huyo baada ya kupoma ameimba wimbo wa Ni wewe.
Riyama aliwafuata na kuwaambia amefurahishwa kuwaona Ommy Dimpoz na Steve Nyerere wakiwa pamoja, kwani ameamini habari nyingi za mitandao huwa zinachochea vitu ambavyo sio vya ukweli kama ilivyokuwa ikidaiwa kuwa wana bifu.
Kutokana na hali hiyo Riyama aliamua kumwambia Steve asimamie msiba wake siku atakapofariki na michango achangishe yeye na fedha za michango zikibaki azichukue.
"Hii nasema kabisa wala si utani, siku ikitokea nimefariki, Steve naomba msiba wangu uchangishe mchango na fedha zikibaki ruksa kuzichukua zote, maana katika hili huwa unafanya kazi nzuri na ya uhakika."