Ndoa ya Lulu na Majizo Novemba 2

Muktasari:

Wawili hawa waliovalishana pete ya uchumba miaka miwili iliyopita, wamekuwa gumzo huko mitandaoni tangu wafanye kitendo hicho huku baadhi ya watu wakiwa wanawauliza mara kwa mara ndoa lini

Hayawi hayawi sasa yamekuwa!hivyo ndivyo unavyoweza kusema kwa msanii Lulu na mpenzi wake Francis Siza maarufu kwa jina la Majizo baada ya kubainika kuwa watafunga rasmi Ndoa, Novemba 2 mwaka huu.

Hayo yamebainika leo Ijumaa Oktoba 23,2020 kutoka kwa mtu wa karibu na Lulu, alipozungumza na Mwanaspoti.

Kama vile haitoshi jana kupitia ukarasa wake katika mtandao a kijamii wa Instagram, Majizo aliweka picha iliyosindikizwa na maeneno’Vile navyoiangalia November 2.... I can’t wait,”.

Wawili hawa waliovalishana pete ya uchumba miaka miwili iliyopita, wamekuwa gumzo huko mitandaoni tangu wafanye kitendo hicho huku baadhi ya watu wakiwa wanawauliza mara kwa mara ndoa lini.

Maswali hayo kwa wakati mwingine yalionekana mwiba kwa Lulu na alikuwa akiwapa majibu ya hapa na pale ilimradi kuwasuuza nafsi waulizaji kuwa bibi harusi mtarajiwa anawasoma.

Wakati hali ikiwa hivyo, moja ya mtu wa karibu wa Lulu ambaye jina lake halisi ni Elizabeth Michael, ameidokeza Mwanaspoti kwamba ndoa ya wawili hao tayari imefahamika itafanyika Novemba 2 mwaka huu na kuwataka watu wakae mkao wa kula.

“Nyie kaeni mkao wa kula, harusi mliyokuwa mnaisubiri ni Novemba 2, mwaka huu na tayari vikao vya ndugu, jamaa na marafiki wa karibu vimeshaanza,”kimesema chanzo hicho.

Hata hivyo wiki mbili zilizopita kumekuwepo na taarifa za kutangazwa kwa ndoa hiyo katika kanisa la Mtakatifu Andrea, Lililopo maeneo ya bahari Beach, Kata ya Ununio Jijini Dar es Salaam na Jumapili ya keshokutwa inaelezwa kuwa ya mwisho ya kutoa tangazo hilo.