Nandy afunga mjadala ndoa yake na Ruge

Muktasari:

Nandy amaliza mjadala kuhusu uhusiano wake na Ruge asema walitarajia kufunga ndoa Machi mwaka huu

Msanii wa muziki wa kizazi kipya Faustina Charles maarufu kama Nandy ameweka wazi kuhusu uhusiano wake na aliyekuwa Mkurugenzi wa vipindi wa Clouds Media Group, marehemu Ruge Mutahaba na kueleza kuwa walipanga kufunga ndoa Machi mwaka huu.

Akihojiwa na Millard Ayo, Nandy ameeleza uhusiano wao ulikuwa wa siri kwa kuwa walikubaliana kulifanya suala hilo kuwa lao binafsi.

Amesema kuwa mara kadhaa alikuwa akikanusha kuhusu uhusiano huo kwa kuwa waliona hakuna haja ya kuweka wazi.

“Hatukupenda uhusiano wetu uendeshwe na mitandao, tulikuwa tunajaribu kutengeneza njia ya maisha yetu binafsi ili kufikia lengo letu. Hatukutaka life style ya mahusiano ya awali ya Ruge yajitokeze kwenye maisha yetu.”

Nandy ameeleza kuwa uhusiano wao ulianza baada ya yeye kuanza kumshirikisha Ruge katika vitu vingi na uhusiano wao ulipoanza familia zao zote zilikuwa zikifahamu.