NANDY: Afichua siri ya penzi la staa Kenya

KAMA kuna msanii aliyekata kiu ya mashabiki kumkosa Rehema Chalamila (Ray C) ama Recho basi ni Faustina Charles Mfinanga a.k.a Nandy, ambaye kwa sasa ameishika game ya Bongo Flava kinoma.

Nandy, ambaye ameitengeneza a.k.a yake kutoka kwenye jina la kiasili la jina la Kipare, Nandera, ameibuka kuwa msanii wa kike mwenye umri mdogo lakini aliyefanikiwa kuwakamata mashabiki katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Staa huyu kama ilivyo kwa wengine, alianzia kuimba kanisani wakati huo akiwa na miaka 5 na kwaya ya watoto kwenye Kanisa la KKKT mjini Moshi, limechangia sehemu kubwa kukuza na kuendeleza kipaji cha Nandy.

Mbali na kanisani, pia vipindi vya kuimba na maigizo pale Shule ya Msingi Mawenzi na baadaye Sekondari ya Lomwe, vimemfanya Nandy kuwa huyu anayesumbua na ngoma za Nonogeshe, I’m Confident, Nagusa gusa, One Day, Wasikudanye, Kivuruge na Aibu.

Ngoma hizo ndio zimemfanya Nandy kupasua anga na kufanya kazi na wasanii wakubwa kule Kenya, akiwemo staa wa injili anayebamba kinoma kwa sasa, Willy Pozee.

Nandy ameshirikishwa na Willy Pozee kwenye ngoma ya Njiwa ambayo kule Kenya imekuwa ikikonga nyoyo za mashabiki na kumfanya kuongeza idadi ya wafuasi wake nje ya Tanzania.

VIPI KWA POZEE?

Kukamata kwa ngoma ya Njiwa hakujamuwacha salama Nandy kwani, ghafla tu zikashika taarifa kuwa wawili hawa wana mahusiano yalivuka mipaka kutokana na kunaswa kona mbalimbali.

Hata hivyo, Nandy ambaye ni msomo mwenye taalamu ya biashara kutoka Chuo cha Biashara (CBE) Dar es Salaam na tunda la kituo cha Tanzania House of Talent (THT), akazisikia na fasta tu akafunguka.

Nandy aliyeanza kutamba na ngoma yake ya Nagusagusa akiwa imepikwa na Ema the boy, amesema amekuwa karibu na Pozee kama ilivyo kwa wasanii wengine kama ilivyo kwa Aslay.

Habari za Nandy kuonekana maeneo na Willy Pozee zimeshika kasi zaidi kule jijini Nairobi, Kenya, baada ya msanii huyo kuonekana kuwa na ukaribu wa kupitiliza na picha za pamoja kusambaa kwenye mitandao mwishoni mwa mwaka jana.

Picha hizo, nyingi walionekana kwenye mapozi tofauti ya kichokozi na kuwafanya mashabiki wengi kuamini kwamba, kuna jambo linaendelea kwa wawili hawa.

Hata hivyo, Nandy ambaye hivi karibuni alikuwa jijini Nairobi, amekanusha kuwepo kwa uhusiano wa kimapenzi kati yake na Pozee na kueleza kuwa, ilikuwa ni kwa ajili ya kazi tu.

“Hamna kitu kati ya mimi na Pozee. Unajua mimi ni msanii wa kike hivyo nikifanya kazi na mwanamume lazima mtu aanze kushuku na kuhoji kunani?

“Yeye sio wa kwanza kuwekewa shauku. Nimefanya kazi na (Dogo) Slay nikienda kwenye interview naulizwa, kwani nyinyi na Aslay mna nini? So hamna kitu chochote,” Nandy alifafanua Nandy, ambaye anatamba na ngoma mpya ya Hazipo inayosumbua kila kona ya burudani.

Kuhusu hizo picha za kizushi ambazo walitupia sana mwaka jana, Nandy alisema zililenga kupromoti ngoma ya Njiwa.