Mrembo wa Tanzania ashinda taji la dunia la Miss Landscape

Muktasari:

Fainali aliingia na warembo wa Marekani, Poland na Colombia.

Dar es Salaam. Mwakilishi wa Tanzania mashindano ya Miss Landscape ya dunia, Anitha Mlay ameibuka mshindi wa pili, huku nafasi ya kwanza ikichukuliwa na mrembo wa Marekani.

Anitha ameibuka kidedea nyuma ya mrembo wa Colombia aliyeshika nafasi ya tatu huku ya nne ikibebwa na Poland.

Anitha anayesoma stashahada ya sheria, amepeperusha vyema bendera ya Tanzania katika fainali za mashindano hayo zilizofanyika jana, Juni 5, 2019.

Shindano hilo la urembo la kimataifa linalobeba kampeni za utunzaji mazingira, kupiga vita ujangili pamoja na kutangaza utalii limeshirikisha warembo kutoka mataifa 41.

Mratibu wa mashindano hayo nchini, Happy Maina amesema lengo kuu la Kushiriki katika Miss Landscape International ni kujishirikisha katika maswala ya jamii, kama utunzaji mazingira pia kutumia fursa hii kuitangaza nchi kimataifa.

“Naamini ushindi wa Anitha ni wa Taifa. Tumefurahi kuona bendera ya nchi yetu imepeperushwa hasa kwa kuona mrembo wetu ameweza kuchuana na wa Marekani mpaka hatua ya mwisho. Hili ni jambo la kihistoria na kujivunia,” amefafanua Maina.