Luiza: Ajali tuliyopata ni Mungu tu

Muktasari:

  • Wanamuziki wa Bendi ya Twanga pepeta wamepata ajali wiki iliyopita na jana walienda Hospitali ya muhimbili kwa ajili ya vipimo zaidi.

Dar es Salaam. Siku tatu baada ya kusalimika katika ajali ya gari, mwanamuziki Luiza Mbutu amesema kunusurika kwao ni Mungu tu.

Luiza amesema ajali iliyotokea juzi gari walilokuwa wamepanda kuharibiwa vibaya hawakutarajia kama wangetoka salama.

Liuza akiwa na wasanii wenzake Supa Nyamwela, Jojoo Jumanne, Luwa Luwa akiwemo na dereva wa gari hiyo Hilary walipata ajali Feb 3, 2019 saa 10 alfajiri, maeneo ya Mwenge Mataa.

Chanzo cha ajali hiyo kimetajwa kuwa ni uzembe wa dereva wa gari iliyokuwa ikitokea Barabara ya Coca-Cola, kutoheshimu taa za makutano ya Barabara ya Bagamoyo na Sam Nujoma eneo la Mwenge Dar es Salaam.

Gari walilokuwemo wanamuziki hao lilipinduka mara tatu huku gari lililosababisha ajali lilikimbia baada ya kugonga, hata hivyo kibao cha namba ya gari hiyo kilidondoka.

Luiza alisema anashukuru Mungu na wanaendelea vizuri kiasi, na jana Mkurugenzi wao wa Bendi ya Twanga Pepeta, Asha Baraka aliwapeleka Hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya kupata vipimo zaidi, kwani yeye bado anamaumivu kichwani huku Nyamwela bado anamaumivu ya kichwa na mkono.

"Nawashukuru sana ndugu zangu, mashabiki wetu wote waliotupa pole,kwa sasa tunaendelea vizuri kiasi, kwani mimi nina maumivu makali kichwani na shingoni na Nyamwela anamaumivu ya kichwa na mkono begani, na jana Mkurugenzi wetu Asha Baraka alitupeleka Hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya vipimo tunaendelea na dawa na tumeambiwa tupumzike kazi kwa wiki mbili zipite," alisema Luiza.