Kumbe Wema mbwembwe tu!

MASHABIKI wa mwanadada mwenye mvuto wa kipekee Bongo, Wema Sepetu, kazi anayo. Mashabiki wake wamemjia juu baada ya kauli yake kwamba mwaka mpya utakuwa wa mafanikio kwake.

Wema ambaye ni Miss Tanzania wa mwaka 2006 na pia mwigizaji wa filamu za Bongo Movie, amenangwa vikali na mashabiki hao katika mitandao ya kijamii wakisema wamechoshwa na kauli hiyo anayowapa kila unapofika mwaka mpya, lakini hawajawahi kuyaona hayo mafanikio anayoyasema.

Wamesema kila ifikapo Desemba huwa anataja malengo na kusema atayafanyia kazi mwaka mpya, lakini mwaka ukifika hakuna kinachofanyika zaidi ya kuanza upya na skendo za hapa na pale.

“Nampenda sana Wema, ila wakati mwingine anaboa na ahadi zake za kila wakati, mfano hadi leo nasubiri movie (filamu) ya Day After Death. Huu ni mwaka wanne sasa tangu alipoahidi kuitoa,” alisema Yasinta, mmoja wa mashabiki wake.

“Tumemchoka bana, tatizo ukifika muda aliopanga anajisahau na kuingiza drama (maigizo) zake na kupoteza yale aliyopanga. Inabidi Wema abadilike, malengo anayojiwekea kuhusu mwaka mpya kama akiyatekeleza anaweza kufika mbali,” anaongeza shabiki mwingine, Joseph.