Kivuli cha Mangwair bado kinamtesa Bushoke

Muktasari:

  •  Nimegundua ni kila enzi ina muziki wake na mambo yake ingawa ni vyema zikafanyika kazi zile ambazo zitaishi kwenye mioyo ya watu na zitakuwa funzo na burudani 

Dar es Salaam. Mwanamuziki Luta Bushoke amesema marehemu Albert Mangwair ameondoka na ubunifu wake na kudai alifanya muziki wake kwa ajili ya mahitaji ya jamii.

Bushoke anasema kuna wakati analitazama gemu la muziki na kubaini kuna aina fulani ya ladha zinapotea kwa madai wapo wasanii ambao walifanya vitu baadhi wamefariki na wengine wameamua kunyamaza na kuangalia kinachoendelea.

 "Mangwair alikuwa kichwa kwa maana ya akili nyingi ambayo ilifanya kazi zake ziwe na ujumbe kwa jamii, nakumbuka uwepo wake kama najiulize angekuwepo huenda angefanya kitu kikubwa kwenye gemu hii.

"Sina maana kwamba wanaovuma kwa sasa wanafanya vibaya, niligundua ni kila enzi ina muziki wake na mambo yake ingawa ni vyema zikafanyika kazi zile ambazo zitaishi kwenye mioyo ya watu na zitakuwa funzo na burudani.

"Muziki upo kwa ajili ya watu, hivyo kuna haja ya kufanya utafiti wa kujua hao watu wanahitaji nini, binafsi naona kabisa Mangwair alikuwa na aina yake ya uimbaji ambayo iliwavutia wengi," anasema.

Mbali na ishu za muziki Bushoke ni shabiki kindaki ndaki wa Yanga, ameushauri uongozi wa klabu hiyo kufanya usajili wa maana ili msimu ujao uwe wa mafanikio ya kutwaa taji la ligi.

"Yanga ni klabu kubwa inatakiwa kupigania ubingwa ingawa hata kumaliza nafasi ya pili imejitahidi kutokana na hali halisi ilivyokuwa," anasema.