Juma Nature afunguka ajali msafara wa Nandy Festival

Muktasari:

  • Jana usiku katika mitandao ya kijamii kulizagaa taarifa gari lililokuwa limewabeba wasanii Juma Nature, Whozu, Stamina, Nandy, Barnaba, Roma, Billnass, Ice Boy na Willy Paul likielekea Sumbawanga, lilipata ajali katika eneo la Mikumi, mkoani Morogoro

Dar es Salaam. Mwanamuziki wa Bongo Flava, Juma Nature amesema ajali iliyotokea katika msafara wa Nandy Festival ulihusisha gari lililobeba vyombo vya muziki na baadhi ya wacheza shoo hawakupata majeraha makubwa.

Jana usiku katika mitandao ya kijamii kulizagaa taarifa gari lililokuwa limewabeba wasanii Juma Nature, Whozu, Stamina, Nandy, Barnaba, Roma, Billnass, Ice Boy na Willy Paul likielekea Sumbawanga, lilipata ajali katika eneo la Mikumi, mkoani Morogoro.

Akizungumza na MCL Didital leo Juni 4, Juma Nature ‘Kibra’ amesema ajali ikitokea kila mtu huwa anaongea neno lake, ila ukweli ni kwamba wasanii wote wapo salama gari lililobeba vyombo vya muziki na baadhi ya wacheza shoo na wapiga vyombo ndilo lililopata ajali.

“Unajua kila mtu anaongea la kwake, ukweli gari la wasanii halikupata ajali ila lililopata ni gari lililobeba vyombo ambalo tulikuwa nalo katika msafara wa Nandy Festival.”

Naye, Nandy katika ukurasa wake wa Instagram ametuma kipande cha video kinachoelezea waliopata ajali ni wale waliokuwa katika gari lililobeba viongozi, wapiga vyombo vya muziki na wacheza shoo, na kwamba baadhi ya majeruhi wamesafirishwa kwenda Dar es Salaam.