Irene Uwoya : Hajafulia mtu , ukiniganda tu umeumia

Muktasari:

Mwanaspoti lilipata nafasi ya kupiga naye stori lilipoibuka ilipo baa yake iitwayo Last Minute maeneo ya Sinza Mori, jijini Dar es Salaam na amefunguka yote kuhusu kudaiwa amefulia na mambo mengine ambayo huyajui kuhusu yeye.... huyu hapa.

MAISHA ni vile unavyoishi. Ukiwa supastaa kufuatiliwa ni lazima. Hata hivyo, sio wote, wengine hawapendi maisha hayo na wanataka kuishi maisha ya kawaida kama raia wengine, lakini kuna wale kila kukicha wanaishi machoni mwa watu kupitia mitandao ya kijamii, magazetini, kwenye runinga na hata redioni. Kwa kifupi, maisha yao ni kwenye vyombo vya habari.

Tofauti na unavyomfikiria nyota wa filamu ‘Bongo Movie’ nchini, Irene Uwoya. Amekuwa akiposti mambo yake mengi mitandaoni na hasa Instagram, lakini ghafla tu mapema mwezi Januari akaamua kuacha.

Hatua hiyo imewapa watu maswali na wengi kuhisi huenda amefulia na maisha yamempiga kabali.Hata hivyo, mwenyewe anasema wanaofikiria hivyo ni washamba wa maisha na wajue tu utajiri haupo mitandaoni na ukimya wake huko haimaanishi amefulia.

Mwanaspoti lilipata nafasi ya kupiga naye stori lilipoibuka ilipo baa yake iitwayo Last Minute maeneo ya Sinza Mori, jijini Dar es Salaam na amefunguka yote kuhusu kudaiwa amefulia na mambo mengine ambayo huyajui kuhusu yeye.... huyu hapa.

UKIMYA WAKE VIPI?

Irene anasema kuwa kimya kwa mtu si kuishiwa na kama watu wanaishi maisha ya kuangalia wasanii kwenye mitandao wanaposti nini ndio wajue ana pesa au hana, inabidi waelimike, kwani maisha ya mtandaoni asilimia kubwa ya watu ni feki. Kwenye akaunti yake ya Instagram inayofahamika kama Ireneuwoya8, anasema imekumbwa na janga na tangu Januari 4, mwaka huu hajaposti kitu ndio maana watu wasiofahamu hilo wanadai yupo kimya kwa sababu amefulia.

“Unajua mashabiki wamekuwa na fikra potofu, wanapoona msanii yupo kimya akili zao zinawatuma kaishiwa wakati sivyo, sasa mimi kutoonekana mitandaoni kumeleta shida watu wanachonga sana nimefulia mara nini, nawaonea huruma wale wenye kujaji maisha ya watu mtandaoni maana asilimia kubwa yanakuwa feki. Sasa Mimi kutokuposti kitu au kutoposti nakula bata watu wanaanza kuunda maneno ya kufulia, kiufupi huko wanakoangalia akaunti yangu ya Ireneuwoya8 imekumbwa na tatizo ndio maana sijaposti kitu tangu Januari, kwa sasa natumia ireneuwoya8_backup wanitafute huko waache uswahili wao,” anasema Uwoya

KAFULIA? MSIKIE HAPA

Aidha Uwoya aliendelea kusema kimya si kuishiwa, watu wamekuwa wakimsema sana lakini hataki kuwajibu kwa kuwa anajua nini anafanya na hakuna anayemwongoza maisha yake, ila anashangaa watu kujipa kibarua cha bila malipo kumfuatilia kwenye mambo yasiyo na maana. “Watu wanasema sana juu yangu, lakini mimi sitaki kuwajibu kwa kuwa najua hawajui wasemalo, kwanza nifulie nisifulie wao haiwahusu, ila ukweli utabaki hawawezi kujua maisha yangu na wala sitaishi watakavyo wao bali nitakavyo mwenyewe.

”Na kama mtu kuwa na pesa anaonekana tu mtandaoni akiposti kitu basi akili za watu hazina uwezo wa kufikiri, kukaa kimya kwenye mitandao hakumaanishi mtu kufulia, japokuwa kama nilivyosema, sipo kimya mtandaoni ila natumia akaunti nyingine kwa sasa,” anasema Uwoya.

MWANAMUME ASIMGANDE,ITAKULA KWAKE

Uwoya ameshatoka kimapenzi na wanaume mbalimbali akiwamo aliyekuwa mumewe marehemu Hamadi Ndikumana na msanii wa Bongo Flava, Dogo Janja. Wote hao na wengine wameishia kutemana naye. Kifupi anasema hapendi mwanamume amgande.

Kwa sasa kinachozungumzwa ni ishu yake ya kuachana na mwanamume aliyekuwa anamhudumia kwa kumpa hela na wengi wanadai kuachana kwake na wanaume ni kwa sababu yeye ni mkorofi.

“Nakujibu swali la mimi mkorofi ndio maana sidumu na wanaume, hilo la kuachana na mwanamume mwenye pesa sijui, achana nalo kwani ndio limezua hizo habari za kuambiwa niko kimya mtandaoni kisa nimeachwa na mwanamume anayenipa pesa, watasubiri sana hilo.

“Hilo swali la mimi mkorofi sio kweli kabisa, sema mimi ndivyo nilivyo halafu sitaki mwanamume anigande kiivyo, kwa sababu siyo ndugu yangu, ndiyo maana sidumu na wapenzi na kuambiwa mkorofi,” anasema Uwoya.