Dudubaya asamehewa

Muktasari:

Serikali ta Tanzania imemsamehe msanii, Godfrey Tumaini maarufu Dudubaya baada ya kumfungia kwa muda usiojulikana kujihusisha na kazi za sanaa.

Dar es Salaam. Serikali ta Tanzania imemsamehe msanii, Godfrey Tumaini maarufu Dudubaya baada ya kumfungia kwa muda usiojulikana kujihusisha na kazi za sanaa.

 

Alifungiwa na Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) baada ya kukataa wito kuhojiwa kuhusu tuhuma alizozitoa katika mitandao ya kijamii kuhusu sanaa.

 

Baraza hilo limeeleza kuwa Dudubaya alitumia lugha zisizo na maadili.

 

Hata hivyo, Januari 23, 2020 Dudubaya alijisalimisha Basata  na kuomba msamaha lakini baraza hilo halikutoa uamuzi wowote kwa kuwa mamlaka ya kufanya hivyo ipo chini ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

 

Jana Jumanne Februari 11, 2020 msani huyo alikwenda katika ofisi za Waziri wa wizara hiyo, Dk Harrison Mwakyembe kuweka mambo sawa.

 

Leo Jumatano Februari 12, 2020 katibu mtendaji wa baraza hilo, Godfrey Mngereza amesema Dudubaya amesamehewa baada ya kusikilizwa na Dk Mwakyembe.

 

Amesema Basata haikuwa na mamlaka ya kumfungia na aliandika barua ya kukata rufaa kwa waziri, “sheria ya baraza namba 23 ya mwaka 1984 na marekebisho yake yaliyofanywa mwaka 2006 inaeleza mtu yeyote akipewa adhabu na Baraza, sheria inampa nafasi ya kwenda kumuona Waziri na anachosema Waziri ndicho kitakachotekelezwa.”

 

Mngereza amewataka wasanii kuzingatia sheria kanuni na taratibu, “wasanii wana nguvu kubwa, wanapaswa kuishi kwa kufuta maadili kwani watu wengi wanawafuatisha wakiwemo watoto, pia haileti picha nzuri katika sanaa ikizingatiwa kuwa ni moja ya kipengele kinachoitambulisha nchi.”