Bi Cheka afariki duniani hospitali ya Mloganzila

Muktasari:

Aidha Temba amesema atamkumbuka Bi Cheka kwa ucheshi wake, ukarimu na kupenda muziki bila kuangalia umri aliokuwa nao.

Dar es Salaam. Mwimbaji aliyewahi kutamba katika ya Kundi la Wanaume Familiy, Cheka Haji 'Bi Cheka' amefariki dunia leo katika Hospitali ya Mloganzila.

Akizungumza na Mwanaspoti, Mheshimiwa Temba amesema, Bi cheka amefariki akiwa anasumbuliwa na tatizo la moyo.

"Ni kweli Bi Cheka amefariki, mara ya mwisho mimi kuongea naye ilikuwa miezi mitano iliyopita, nilipigiwa simu na mwanamke mmoja kunipa taarifa kuwa anaumwa,”

"Wakati huo mimi nilikuwa Mkoani, nikawaambia nikirudi nitaenda kumuona, kiukweli sijaenda kumuona kutokana na kutingwa na shughuli za hapa na pale," alisema Mheshimiwa Temba.

Aidha Temba amesema atamkumbuka Bi Cheka kwa ucheshi wake, ukarimu na kupenda muziki bila kuangalia umri aliokuwa nao.

Mwaka 2012 tasnia ya muziki wa Bongo Fleva ilivamiwa na mhenga Bi Cheka na kutishia wasanii mbalimbali chipukizi.

Msanii huyo mkongwe aliachia wimbo wake wa 'Ni Wewe' ambao alimshirikisha Mh Temba uliteka katika chati mbalimbali za muziki wa Bongo Fleva.